Home Habari za michezo PAMOJA YA KUWAPIGA WAETHIOPIA KWAO JUZI…GAMONDI ‘ATEMA CHECHE’ YANGA…

PAMOJA YA KUWAPIGA WAETHIOPIA KWAO JUZI…GAMONDI ‘ATEMA CHECHE’ YANGA…

Yanga SC

WASHAMBULIAJI wa Yanga wamejichongea kwa Kocha wao, Miguel Gamondi ambapo ameweka wazi kuwa anahitaji kupata muda wa kuzungumza na safu hiyo ya ushambuliaji baada ya matokeo ya mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya CBE SA ya Ethiopia ambapo Yanga ilishinda kwa 1-0.

Safu ya ushambuliaji ya Yanga inaongozwa na Prince Dube, Jean Baleke, Kennedy Musonda, Clemente Mzize na Stephane Aziz Ki msimu uliopita aliibuka safu bora ya  ufungaji .

Kocha Gamondi ameanza kufanyia kazi kwa kuwapa proglamu ya mazoezi washambuliaji hao wanapokuwa uwanja wa mazoezi ili kutengeneza nafasi kuwa mabao katika mchezo wa marudiani dhidi ya CBE SA.

Yanga watakuwa wenyeji katika mchezo huo utakaopigwa Septemba 21, katika uwanja wa New Amaan, Visiwani Zanzibar, wakihitaji kupata ushindi mkubwa na kufuzu kucheza hatua ya makundi ya michuano hiyo.

Yanga juzi ilifanikiwa kupata ushindi wa bao 1-0 katika mchezo wa hatua ya pili ya Ligi ya Mabingwa Afrika ugenini dhidi ya CBE SA ya Ethiopia na kutengeneza nafasi nyingi na kushindwa kuzitumia.

Katika mchezo huo Yanga ilitengeneza nafasi zaidi ya Sita kwa nyota wake Stephane Aziz Ki, Pacome Zouzoua, Clement Mzize na Prince Dube aliyepatia timu hiyo bao la ushindi dakika ya 45 ya kipindi cha kwanza.

Gamondi amesema anawapongeza wachezaji wake kupambana kwa kufanikiwa kupata ushindi, ana kazi ya kufanya kwenye safu ya ushambuliaji katika suala la kumaliza .

“Tumekosa utulivu tunapokuwa kwenye eneo la mpinzani, tumetengeneza nafasi nyingi tungetulia ninaimani tungefunga idadi kubwa ya mabao ugenini.

Tumerejea nyumbani tunaenda kufanyia kazi mapungufu yetu, kuwapa program washambuliaji kujiandaa na mechi yetu ya marudiano ambayo tunacheza kwenye uwanja wetu na tunahitaju kupata idadi kubwa ya mabao,” amesema Gamondi.

Naye Rais wa Yanga, Hersi Said amesema wachezaji wamepambana, kupata bao moja ugenini mwanzo mzuri, kocha Gamondi ameona mapungufu ya safu ya ushambuliaji na kufanyia kazi kwa ajili ya kupata matokeo mazuri uwanja wa nyumbani.

“Ni mwanzo mzuri kwa kwetu kutafuta tiketi ya kucheza makundi, kwa Altitude 2500 sio rahisi kufanya kile ambacho kilikuwa kinatarajiwa, tumerudi nyumbani kocha anaenda kufanyia kazi madhaifu yote,” amesema Hersi.

Ameeleza kazi kubwa ilikuwa ni kutumia nafasi wanazotengeneza kuwa mabao na kocha ameliona hili anafanyia kazi na mechi ijayo Visiwani Zanzibar anaimani watapata ushindi mnono.

SOMA NA HII  BEKI ALIYEKUWA ANAWINDWA NA YANGA AMALIZANA NA SIMBA