Home Habari za michezo WANAOTAKA KUTUSUA KIMATAIFA….HUU HAPA USHAURI WA MSUVA KWA MASTAA WA KIBONGO…

WANAOTAKA KUTUSUA KIMATAIFA….HUU HAPA USHAURI WA MSUVA KWA MASTAA WA KIBONGO…

Habari za Michezo leo

NYOTA wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Simon Msuva, amesema ushindani mkubwa uliopo kwenye Ligi Kuu ya Tanzania unawalazimu wachezaji wazawa kuongeza bidii ili kupata nafasi katika vikosi vya kwanza vya timu zao.

Msuva amesema ongezeko la wachezaji wa kigeni kwenye ligi limeiboresha kwa kiwango kikubwa, na limeifanya kuwa kivutio si tu kwa mashabiki, bali pia kwa vipaji vya kimataifa vinavyotamani kuonyesha uwezo wao.

“Miaka tuliyocheza sisi na sasa ni tofauti kabisa,” amesema Msuva. “Sasa hivi kuna wachezaji wengi wa kigeni wanaokuja na wanacheza kwa kiwango cha juu. Hii inamaanisha sisi wazawa tunapaswa kupambana zaidi, kujituma uwanjani, na kumshawishi kocha atupatie nafasi.”

Msuva ambaye aliwahi kung’ara na klabu ya Yanga, kabla ya kupata dili la kujiunga na timu mbalimbali nje ya Tanzania kama vile Wydad AC ya Morocco, kwa sasa anakipiga katika klabu ya Al Talaba SC ya Iraq.

Amewataka wachezaji wa Kitanzania kutumia kila fursa wanayopewa iwe ni kwenye mazoezi au mechi kuthibitisha ubora wao na kujihakikishia nafasi katika vikosi vya kwanza.

“Kocha anaangalia nidhamu, bidii, na matokeo ya uwanjani. Ukipata nafasi, iwe ni dakika tano au tisini, lazima uonyeshe thamani yako,” ameongeza.

Kwa sasa, Msuva ni miongoni mwa wachezaji waliobeba jina la Tanzania kimataifa, na anaendelea kuwa mfano kwa vijana wengi wanaotamani kufikia mafanikio kwenye soka.

SOMA NA HII  KIROHO SAFI TU.....AZAM FC WAKUBALI KUACHANA NA DUBE....MASHARTI YAO KWA YANGA NI HAYA TU...