Home Habari za michezo SIKU 6 KABLA YA KUKIPIGA NA YANGA…PIGO JINGINE SIMBA HILI HAPA……

SIKU 6 KABLA YA KUKIPIGA NA YANGA…PIGO JINGINE SIMBA HILI HAPA……

Habari za Simba leo

SIMBA iko uwanjani leo Jumatano kwa mara ya kwanza tangu itoke kambini Misri, lakini baada ya mshambuliaji Jonathan Sowah, kuna staa mwingine inaweza kumkosa mbele ya Yanga.

Simba itamkosa Sowah kwenye mchezo wa Ngao ya Jamii dhidi ya Yanga, lakini mashabiki wa timu hiyo watamuona mshambuliaji huyo raia wa Ghana kwenye mchezo wa leo wa Tamasha la Simba Day.

Sowah ataikosa mechi ya Ngao ya Jamii dhidi ya Yanga baada ya kufungiwa kufuatia kadi nyekundu aliyoonyeshwa kwenye mchezo wa fainali ya Kombe la FA msimu uliopita wakati akiwa na Singida Black Stars.

Baada ya Simba Day leo, Septemba 16, 2025 Simba itakutana na Yanga kwenye mchezo wa Ngao ya Jamii utakaochezwa kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam. Wakati leo Simba ikiadhimisha Tamasha la Simba Day pale Uwanja wa Benjamin Mkapa, taarifa mbaya ni kukosekana kwa kiungo wao mpya Mohammed Bajaber.

Taarifa kutoka Simba ni, Bajaber aliumia tangu akiwa nchini Misri kwenye kambi ya wekundu hao iliyohitimishwa Agosti 28 mwaka huu.

Staa huyo aliyesajiliwa na Simba kutoka Kenya Police FC ya Kenya, ataukosa pia mchezo wa leo wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya Gor Mahia kutoka Kenya kutokana na majeraha hayo.

Kiungo huyo ambaye licha ya leo kutambulishwa lakini anatarajiwa kutocheza mechi hiyo ya kirafiki, atakuwa staa wa pili kuikosa mechi dhidi ya Yanga akitanguliwa na Sowah. Kocha wa Simba, Fadlu Davids alithibitisha kukosekana kwa Bajaber na kikosi chake kitaendelea kumsubiri kiungo huyo ambaye anaamini kipaji chake kitakuwa msaada muhimu kwenye timu yao kwa msimu ujao

“Tutamkosa Bajaber kwenye mchezo wa kesho (leo) kutokana na majeraha, nadhani tunatakiwa kumsubiri kwa wiki chache ili awe sawa,” alisema Fadlu.

SOMA NA HII  KOCHA WA ORLANDO AIPIGA MKWARA SIMBA...ADAI ANAIJUA NNJE NDANI...'ACHA WAJE KICHWA KICHWA'...