LICHA ya ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya TRA United, Kocha Mkuu wa Simba, Steve Barker, ameibua hali ya taharuki ndani ya kikosi chake baada ya kuweka wazi kuwa hakuna nafasi ya kuridhika na kiwango cha sasa cha timu.
Ushindi huo mkubwa haukumfanya kocha huyo kupunguza presha, badala yake ametaka wachezaji wake kuendelea kufanya kazi kwa bidii zaidi.
Katika mchezo huo uliofanyika kwenye Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Simba ilionesha ubora katika kumiliki mpira na kutengeneza nafasi nyingi, jambo lililowawezesha kupata mabao muhimu matatu.
Kocha huyo ameeleza wazi kwamba, licha ya ushindi, bado kuna mapungufu makubwa ndani ya kikosi chake, anatamani kuona mabadiliko makubwa ya kiuchezaji, hasa kuhakikisha timu inakuwa na uthabiti wa kiwango katika kila mechi inayofuata.
Changamoto zilizobainika ni pamoja na umaliziaji wa nafasi na nidhamu ya wachezaji wanapopoteza mpira. Barker ameonya kuwa kushindwa kushughulikia changamoto hizi kunaweza kuiweka timu katika hatari kubwa zaidi katika michezo ya kimkakati.
“Nafurahi kwa ushindi, lakini bado hatujafika pale ninapotaka. Kila mchezaji anatakiwa kuongeza juhudi na umakini zaidi,” amesema Barker, amesisitiza umuhimu wa kila mmoja kuonesha kiwango cha juu kila wakati.
Barker amesisitiza kuongeza ushindani ndani ya kikosi, hakuna mchezaji ambaye ana nafasi ya uhakika kikosini bila kuonyesha kiwango bora katika mazoezi na mechi, jambo linalolenga kuhakikisha kuwa wachezaji wanabaki na tahadhari na motisha ya kufanya vizuri kila wakati.
Kwa hali hii, Simba inatarajiwa kuendelea kuboresha uchezaji wake huku wapinzani wake wakishuhudia presha inayoongezeka kutoka kwa kocha anayesita kuridhika na matokeo mazuri pekee.