LIVERPOOL, ENGLAND: RIPOTI zinaeleza mshambuliaji wa Liverpool, Mohamed Salah huenda asionekane tena uwanjani Anfield baada ya kupata majeraha.
Nyota huyo, 33, anayetarajiwa kuondoka Liverpool baada ya kuhudumu kwa miaka tisa yenye mafanikio makubwa, alionekana kuaga mashabiki wa Anfield kwa hisia baada ya mechi ya Ligi Kuu England dhidi ya Crystal Palace.
Salah alipata maumivu ya misuli ya nyuma ya paja (hamstring) hali iliyosababisha alale chini kwa muda, kisha akasimama na kuondoka taratibu uwanjani.
Kabla ya kutoka, aligeuka na kupiga makofi kuelekea pande zote za uwanja, akipokea heshima na shangwe kutoka kwa mashabiki.
Liverpool imebakiwa na mechi chache za ligi ambazo ni dhidi ya Manchester United, Chelsea, Aston Villa na Brentford na ilitarajiwa mechi ya mwisho dhidi ya Brentford ndio ingetumika kuagwa kwake rasmi.
Mashabiki wameonyesha hofu jeraha hilo linaweza kumaliza safari yake mapema, wakitamani apate nafasi ya kuaga kwa heshima baada ya kucheza zaidi ya mechi 430 na kufunga mabao zaidi ya 250 akiwa na majogoo hao.
Akizungumzia hali ya staa huyo, Kocha wa Liverpool, Arne Slot amesema: “Tumepata ushindi mwingine, pia jeraha lingine, hiyo imekuwa hadithi ya kawaida msimu huu. Ni mapema kusema ukubwa wake, lakini tunamjua Salah, si rahisi kwake kutoka uwanjani, hivyo inaonyesha kuna kitu.”
Katika mechi hiyo, Alexander Isak na Andy Robertson waliipa Liverpool uongozi wa mabao 2-0 kabla ya mapumziko.
Baada ya jeraha la Salah, Daniel Munoz alifunga bao la kufuatia machozi kwa Palace kabla ya Florian Wirtz kufunga la tatu. Matokeo hayo yaliipeleka Liverpool nafasi ya nne.