Home Habari za michezo YUSUF CHIPPO AKALIA KUTI KAVU MTIBWA SUGAR

YUSUF CHIPPO AKALIA KUTI KAVU MTIBWA SUGAR

0

UONGOZI wa Mtibwa Sugar, uko katika hatua za mwisho za kuachana na kocha mkuu wa timu hiyo, Mkenya Yusuf Chippo ikidaiwa ni kutoridhishwa na mwenendo wa kiuchezaji wa kikosi hicho hadi sasa katika mechi za Ligi Kuu Bara.

Taarifa kutoka ndani ya uongozi wa Mtibwa, zimeliambia Mwanaspoti kwa sasa kocha huyo amewekwa mtu kati na muda wowote atapewa mkono wa kwaheri, hasa baada ya timu hiyo kuchapwa bao 1-0 dhidi ya Dodoma Jiji, Mei 6, 2026.

“Baada ya mechi na Dodoma Jiji, uongozi ulimtaka kukaa pembeni na timu hadi pale uamuzi mwingine utakapofanyika, kuanzia leo atakutana na viongozi wa juu wa klabu ili kujadiliana mustakabili wake kiujumla kikosini,” kilisema chanzo hicho.

Kichapo hicho kwa Mtibwa dhidi ya Dodoma Jiji, kimeifanya timu hiyo kucheza mechi tisa mfululizo za Ligi Kuu Bara bila ya kuonja ladha ya ushindi, tangu mara ya mwisho ilipoichapa Tanzania Prisons mabao 2-1, Februari 2, 2026.

Katika mechi hizo tisa ilizocheza Mtibwa Sugar bila ya ushindi, imepoteza sita na kutoka sare tatu, ikifunga mabao sita na kuruhusu 18, ikiwa ni mwenendo mbaya zaidi kwa kikosi hicho, kuanzia eneo la ushambuliaji hadi lile la kujilinda.

Chippo aliyeachana na Murang’a SEAL ya kwao Kenya tangu Agosti 21, 2025, alijiunga na Mtibwa Novemba 17, 2025, ili kuiongoza akishirikiana na Kocha Msaidizi, Awadh Juma ‘Maniche’, aliyeipandisha Ligi Kuu Bara msimu wa 2024-2025.

Tangu Chippo alipojiunga na timu hiyo Novemba 17, 2025, amekiongoza kikosi hicho katika mechi 16, za Ligi Kuu Bara, akishinda nne, sare sita na kupoteza sita huku kati ya hizo timu imefunga mabao 14 na kuruhusu 22.

Msimu huu Mtibwa imecheza mechi 21 za Ligi Kuu Bara, ikishinda tano, sare nane na kupoteza nane, ikifunga mabao 16 na kuruhusu 25, ikiwa nafasi ya 11 na pointi 23 kwenye msimamo.

Kocha huyo aliyewahi kuzifundisha Pamba Jiji, Coastal Union na TRA United, anakumbukwa na mashabiki wengi hasa baada ya kukiongoza kikosi cha Ulinzi Stars kutwaa mataji matatu mfululizo ya Ligi Kuu ya Kenya ‘KPL’ kati ya 2003 na 2005 na kuhudumu akiwa kocha msaidizi wa Harambee Stars kuanzia 2008 hadi 2011.