Home Habari za michezo PRISCILLA OJO SITAFSIRI MAONI YA WATANZANIA MTANDAONI

PRISCILLA OJO SITAFSIRI MAONI YA WATANZANIA MTANDAONI

0

MUIGIZAJI na mwanamitandao maarufu wa Nigeria,  ambaye ni mke wa msanii wa muziki wa Bongo Fleva, Juma Jux, Priscilla Ojo ameweka wazi msimamo wake kuhusu namna anavyoyasoma na kuyachukulia maoni ya watu kwenye mitandao ya kijamii.

Priscilla, ambaye amejaaliwa mtoto mmoja aitwaye Rakeem tangu wafunge ndoa yao kubwa miaka miwili iliyopita, alisema amechagua njia ya kupuuza kelele ili kulinda amani ya moyo.

Katika mahojiano ya hivi karibuni, Priscilla alielezea anaishi katika mazingira ambayo lazima ajifunze kuishi na watu kwa amani, bila kujali kama wanamkubali au la.

Aliongeza, amani yake ni kipaumbele, hasa ikizingatiwa sasa anaishi Tanzania na anaingiliana na jamii hiyo kila siku.

“Mwishowe ninaishi hapa, kwa hiyo lazima niwe na amani na wakwe zangu na Watanzania iwe wanapenda au la kwa sababu sasa ni sehemu ya jamii hiyo,” alisema Priscilla.

UHUSIANO NA WAKWE ZAKE

Licha ya changamoto za mitandaoni, Priscilla alisema familia ya mume wake walimpokea vizuri na anajihisi kuwa zaidi ya nyumbani licha ya ugeni wake.

“Nadhani familia nzima ni watu wazuri na watulivu na wamekuwa wakitusaidia sana,” alisema Priscilla akionyesha kuridhishwa na namna alivyopokelewa kwenye familia ya msanii huyo anayetamba na kibao cha ‘Joy’ alichoshirikishwa na Diamond Platnumz.

MITANDAONI

Kuhus maneno ya wanaomsema vibaya mitandao, Priscilla amekiri mara nyingi watu wanakuwa na maneno ya kashfa au chuki, lakini amechagua kutowapa kipaumbele.

Aliongeza moja ya vitu vinavyomsaidia ni kutoielewa vizuri lugha ya Kiswahili inayotumika na baadhi ya watu kumshambulia na hapendi kuangalia nini kinasemwa.

“Sitaki kujihusisha kabisa na mambo ya kutafsiri kwa sababu huwa naona maoni ya Watanzania lakini sitafsiri kwa sababu hata nikijua mengine yanaweza kuniumiza hivyo, naacha tu.”