Kwa upande wa nahodha wa Namungo, Jacob Masawe amesema: “Tupo nafasi mbaya kuliko Singida Black Stars kila mechi kwetu ni muhimu kushinda, tumejipanda na tupo tayari kupambana kwa kadri tutakavyoweza.”
TRA VS JKT TANZANIA
Achana na vita ya pointi tatu kufukuzia nafasi nne za juu, utamua wa mchezo wa TRA United dhidi ya JKT Tanzania ni kwa kukutana kwa makocha wa timu hizo, Ettiene Ndayiragije na Ahmad Ally katika sura tofauti.
Makocha hao wanakutana ikiwa ni takribani miaka saba tangu walipofanya kazi pamoja katika kikosi cha KMC mwaka 2019, kabla ya Ndayiragije aliyekuwa kocha mkuu kutimkia Azam na kumuacha msaidizi wake huyo akiendelea na majukumu.
Ndayiragije raia wa Burundi ndiye alimtambulisha rasmi Ahmad katika Ligi Kuu mwaka 2017 alipoamua kumvuta katika kikosi cha Mbao FC akitokea kituo cha michezo cha Marsh Athletes kilichopo mitaa ya Mirongo jijini Mwanza wakati akiinoa Marsh Queens.
Baada ya kufanya kazi kwa mafanikio katika kikosi cha Mbao, Ndayiragije alipata dili la kutua KMC ambapo aliamua kuondoka na benchi lake, akiwamo Ahmad na kocha wa viungo Faraji Muya.
Kocha huyo baada ya kufanya kazi Azam kwa muda mfupi, aliitwa timu ya Taifa ‘Taifa Stars’ kabla ya kuondoka tena nchini kwao kabla ya kujiunga na Police FC ya nchini Kenya na kisha TRA United kumrejesha Tanzania.
Hata hivyo, uhondo wa mchezo huo ambao utapigwa kesho Jumanne kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha, unavuta hisia kali kwa makocha na timu hizo kuwania pointi tatu kujiweka nafasi nne za juu.
Msimu huu TRA United (zamani Tabora United) na JKT Tanzania zimeonekana kuwa na moto mkali kwa ushindani unaooneshwa na wababe hao na kuweka vita ya kusaka nafasi ya kuwakilisha nchi kimataifa mwakani.
Timu hizo zimekuwa bora kwenye mashindano yao msimu huu kwani mbali na kukimbizana kwenye nafasi nne za juu, wababe hao wamefuzu nusu fainali ya Kombe la Shirikisho la CRDB wakiungana na Yanga, Simba, Azam na Mashujaa.
Hadi sasa JKT Tanzania wapo nafasi ya tano kwa pointi 35 wakiwa na wastani wa bao moja, huku wapinzani TRA United wakiwa nafasi ya sita kwa pointi 33 na wastani wa mzuri wa mabao saba ya kufunga.
Akielezea mchezo huo, Ahmad Ally amesema vijana wake wako tayari akieleza kuwa wamejiandaa kiakili, kisaikolojia na kiufundi dhidi ya TRA United akikiri ugumu wake. “Tunaona vita ya pointi kwenye msimamo lakini tuko tayari kwa mchezo huo japokuwa tunafahamu ugumu ila tutaenda kwa mipango dhidi ya wapinzani hao, wachezaji wangu wako imara,” amesema kocha huyo.
Kwa upande wake Ndayiragije amesema malengo yake ni kuitambulisha timu hiyo kwenye mashindano ya kimataifa, akibainisha kuwa kila mchezo kwao ni vita ya pointi tatu ili kufikia ndoto zao.
“Ligi ni ngumu na kila timu inapambana kadiri ya uwezo kutafuta ushindi, hesabu, malengo na ndoto ni kuitambulisha TRA United kimataifa hivyo tupo tayari kwa kila mchezo,” amesema kocha huyo.
Ingawa takwimu zinaonyesha JKT Tanzania imeshinda mara nyingine (nne) inapokutana na TRA, lakini mechi za hivi karibuni TRA imekuwa ngumu kufungika ikiwa nyumbani.
Kwa mechi tano za mwisho TRA United ikiwa nyumbani, timu hiyo imeonyesha kiwango kizuri, imeshinda tatu dhidi ya Azam (4-1), Pamba Jiji (1-0) na Singida Black Stars (2-0), huku sare ikiwa ni dhidi ya Simba na Yanga zote matokeo yakiwa 0-0.
Jambo hilo limemfanya kocha wa JKT Tanzania, Ahmad Ally kusema: “TRA ina timu nzuri na washambuliaji wenye kasi, mfano Ramadhan Salum ‘Chobwedo’ ambaye kwa sasa ana mabao matatu, hivyo tunajua tunacheza na timu ya aina gani.”