Habari za michezo

MAMELODI YAANZA VIZURU HESABU ZA UBINGWA CAF

Vardo May 17, 2026 10:59 pm

MAMELODI Sundowns imepata faida ya kuutumia uwanja wa nyumbani katika mchezo wa kwanza wa fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika uliochezwa leo Jumapili Mei 17, 2026 huko Pretoria nchini Afrika Kusini baada ya kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya AS FAR Rabat ya Morocco.

Baada ya kushindwa kutengeneza nafasi nyingi ndani ya dakika 37 za mwanzo, Sundowns ilifanikiwa kupata bao la kuongoza kupitia kwa beki wa kushoto wa timu ya taifa ya Afrika Kusini, Aubrey Modiba, aliyepiga mpira wa adhabu kutoka umbali wa yadi 25.

Modiba aliamua kutumia nguvu zaidi, jambo lililomshinda kipa wa AS FAR, Ahmed Tagnaouti. Mpira uliingia wavuni kwa kasi huku kipa huyo akifanikiwa kuugusa tu kwa mkono lakini hakuweza kuzuia.Hilo lilikuwa bao la kwanza kwa Modiba ndani ya karibu miaka mitatu, kipindi ambacho pia alipata kadi mbili nyekundu na hata kujifunga bao moja. Moja ya kadi hizo nyekundu aliipata katika mechi ya hatua ya makundi dhidi ya AS FAR msimu uliopita, hivyo huu ulikuwa wakati muhimu kwake kulipa kisasi.

Sundowns ilikaribia kupata bao la pili ambalo lingewaweka kwenye nafasi nzuri zaidi ya kutwaa ubingwa, baada ya Jayden Adams kuchezewa faulo takribani yadi 30 kutoka golini, Teboho Mokoena alipiga mpira wa adhabu kwa nguvu kubwa kama ilivyo kawaida yake, mpira ukagonga mwamba na kurejea uwanjani.

Baada ya ushindi huo, sasa Sundowns inatarajiwa kusafiri hadi Rabat kwa mchezo wa marudiano utakaochezwa Jumapili ijayo, Mei 24, 2026 ikiwa na kitu cha kulinda, na muhimu zaidi, bila kuruhusu bao la ugenini kutoka kwa AS FAR.

Hii ina maana kwamba, iwapo Sundowns itafunga bao moja nchini Morocco, wenyeji wao watalazimika kufunga mabao matatu ili kubadili matokeo hayo jambo ambalo linaonekana kuwa gumu kutokana na namna mchezo wa kwanza ulivyokuwa.

VAR YACHELEWESHA MECHI
Kipindi cha pili kilichelewa kuanza kwa takribani dakika 30 kutokana na hitilafu ya mfumo wa usaidizi wa waamuzi wa video (VAR).

Awali, AS FAR ilikataa kuendelea na mchezo hadi mfumo huo utengenezwe, lakini kadri muda ulivyozidi kwenda waliamua kurejea uwanjani na kuendelea kucheza.

Kwa mujibu wa sheria za CAF, mechi inaweza kuendelea hata kama VAR haifanyi kazi. Hivyo, kama AS FAR wangeendelea kugoma kucheza, walikuwa kwenye hatari ya kupoteza mchezo huo kwa mabao 3-0. Hata hivyo, tukio hilo halikuonekana vizuri kwa waandaaji wa mashindano.

AS FAR ITAPITA NJIA ZA ESPERANCE, TP MAZEMBE?
Mara ya mwisho kwa timu kupindua matokeo na kutwaa ubingwa wa michuano hii baada ya kupoteza mchezo wa kwanza ilikuwa mwaka 2018, wakati Esperance de Tunis ilipoifunga Al Ahly.

Al Ahly ilishinda mchezo wa kwanza mabao 3-1 mjini Alexandria, lakini timu hiyo ya Tunisia ilijibu kwa ushindi wa mabao 3-0 katika mchezo wa marudiano na kutwaa taji kwa jumla ya mabao 4-3.
Kabla ya hapo, mwaka 2009, TP Mazembe ilitwaa ubingwa kwa faida ya bao la ugenini baada ya kupoteza mchezo wa kwanza dhidi ya Heartland FC.

MIGUEL CARDOSO MTEGONI
Kocha huyo alishindwa katika fainali ya mwaka 2024 akiwa na Esperance de Tunis, pia akapoteza fainali ya 2025 akiwa na Mamelodi Sundowns.
Katika fainali zote hizo, Cardoso alimaliza mchezo wa kwanza wa nyumbani kwa sare na kushindwa kupata ushindi ugenini.

Safari hii, ana faida ya ushindi wa nyumbani, mchezo wa marudiano anakwenda akiwa na kitu cha kulinda hali ambayo ni mpya kwa kocha huyo raia wa Ureno. Swali linabaki, je atafanikiwa kutwaa ubingwa wake wa kwanza wa michuano hii, au hadithi itabaki kuwa ileile.

CHAMA AUWASHA MOTO, SIMBA IKITINGA NUSU FAINALI CRDB FEDERATION CUP KILA MZUNGUKO UNAWEZA KUKUTOA NA KUKUPELEKA MBALI