Habari za michezo

RAUNDI YA 17 WPL KINAWAKA LEO

Vardo May 18, 2026 9:37 am

Ligi Kuu ya Wanawake Tanzania itaendelea leo Mei 18 kwa mechi za raundi ya 17, huku Simba Queens, Yanga Princess na JKT Queens zikitarajiwa kushuka dimbani kusaka pointi muhimu katika mbio za ubingwa.

Tausi FC itamenyana na JKT kwenye Uwanja wa KMC Complex. JKT ambao ni miongoni mwa timu zinazowania ubingwa, wanahitaji ushindi ili kuendelea kupunguza gepu la pointi dhidi ya Simba Queens iliyopo kileleni.

Vinara wa ligi, Simba itakuwa nyumbani Uwanja wa KMC Complex Mei 19 kuikaribisha Ruangwa Queens katika mechi inayotarajiwa kuwa muhimu kwa wenyeji wanaotaka kuendelea kuongoza msimamo wa ligi. Timu hiyo inaingia kwenye mchezo huo ikiwa katika kiwango bora baada ya kucheza mechi 16 bila kupoteza.

Yanga Princess, wanaoshika nafasi ya tatu kwenye msimamo, watakuwa wenyeji wa Ceasiaa Queens katika Uwanja wa Azam Complex mechi itakayopigwa Mei 19 saa 12 jioni. Yanga wanapewa nafasi kubwa ya kushinda, lakini watahitaji kuwa makini dhidi ya wapinzani wao wanaopambana kujinasua kutoka chini.

Alliance Girls, timu iliyovutia mashabiki wengi kutokana na ubunifu wao wa kuingia uwanjani wakiwa katika mavazi ya kipekee, watasafiri hadi Karume kuvaana na Bunda Queens katika mechi inayotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa.

Michezo mingine ya raundi hiyo itawakutanisha Fountain Gate Princess dhidi ya Mashujaa Queens kwenye Uwanja wa Tanzanite Kwaraa, huku Bilo FC ikicheza na Geita Queens katika Uwanja wa Nyamagana.

SERENGETI BOYS IMEANZA VIZURI, HAMASA IONGEZWE TUNISIA WATAVUNJA MWIKO KOMBE LA DUNIA