GEIT GOLD JIJI ZAMSAKA KAZI
OFA za kuhitaji huduma ya beki wa kati wa Namungo FC, Hussein Kazi zipo zaidi ya nne, miongoni mwa timu zinazotajwa hadi sasa ni Geita Gold, Kagera Sugar, JKT Tanzania na Coastal Union ya Tanga.
Imeelezwa Kazi anamaliza mkataba wake na Namungo mwisho wa msimu huu, ingawa timu hiyo imempa ofa mpya lakini inaonekana kuna mambo bado hawajakubaliana, huku akiwa na ofa kadhaa mezani kwake.
Kazi ni mmoja kati ya mabeki mahiri kwenye ligi akiwa pia alishaitumikia timu ya Simba kwa msimu huu na kupelekwa Namungo kwa mkopo.
“Kati ya timu hizo zinazofanya mazungumzo ya mara kwa mara na meneja wake ni Geita Gold na Pamba Jiji, lakini hadi sasa hajasaini timu yoyote, wanajipa muda wa kuzichambua ambazo zitakuwa na manufaa kwa mchezaji,” kilisema chanzo hicho na kuongeza;
“Sababu ya kushindwa kumalizana na Namungo anayoichezea kwa sasa ipo kwenye mapambano ya kujiondoa kushuka daraja, inakuwa ngumu kwake kwani hajui kitakachotokea, ndiyo maana hajasaini anahitaji muda zaidi.”
Soka la Bongo lilimtafuta Kazi ili kuthibitisha hilo, alisema kwa sasa anahitaji utulivu, kuweka umakini katika mechi za ligi zilizosalia ili huduma yake iifae timu isishuke.
“Akili yangu, nguvu zangu nimewekeza katika mechi ili kuipambania timu iliyoniajiri kwa sasa, siwezi kuanza kuzungumzia nitaenda wapi kipindi hiki kigumu na chenye presha ya kupambana ili tusishuke daraja,” alisema Kazi.
Namungo ipo nafasi ya 13 katika msimamo wa Ligi Kuu, imecheza mechi 26, imeshinda tano, sare 11, imefungwa 10, imevuna pointi 26, jambo ambalo Kazi alisema hawapo pazuri kila mchezaji anatamani kuhakikisha timu inasalia salama.
Mechi zilizobakia za Namungo ni dhidi ya TRA United, KMC, Fountain Gate na Mtibwa Sugar, jambo ambalo Kazi alisema:”Ukiangalia mechi tulizosalia nazo ni za timu zinazohitaji pointi kama sisi, hivyo siwezi kuwa na nguvu ya kuanza kuhangaika na ofa kwa sasa.”