Home Uncategorized MCHEZO MZIMA WA UBINGWA LIGI KUU BARA UNAISHA NAMNA HII, MAMBO YAKIJIPA...

MCHEZO MZIMA WA UBINGWA LIGI KUU BARA UNAISHA NAMNA HII, MAMBO YAKIJIPA BINGWA ATATANGAZIWA NANGWANDA SIJAONA


MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu Bara, Simba wana nafasi kubwa ya kutetea ubingwa wao msimu huu kutokana na kuwa vinara wakiwa na pointi 71 na kuwakimbiza washindani wao Azam FC na Yanga kwa idadi kubwa ya pointi.
Simba imebakiza mechi tano ili kujihakikishia ubingwa kwani endapo ikishinda mechi hizo itakusanya pointi 15 zitakazofanya wafikishe pointi 86 ambazo hazitafikiwa na wapinzani wao, Azam na Yanga endapo watashinda mechi zao zilizobaki na huenda wakatangazia ubingwa Uwanja wa Nangwanda Sijaona, Mtwara.
Takwimu hizo zimekuja ikiwa ni muda mfupi baada ya Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa kutangaza kusimamisha shughuli zote za michezo na mikusanyiko mingine yoyote ambayo haina umuhimu kutokana na hofu ya kusambaa kwa Virusi vya Corona.

Mechi hizo za Simba zilizosalia katika Ligi Kuu kabla ya kushinda ubingwa ni dhidi ya Ruvu Shooting (Uwanja wa Taifa), Mwadui (Taifa), Mbeya City na Prisons (Sokoine) na Ndanda (Nangwanda Sijaona).
Katika mzunguko wa kwanza, matokeo ya mechi hizo za Simba yalikuwa; Simba 3-0 Ruvu Shooting, Mwadui 1-0 Simba, Simba 4-0 Mbeya City, Simba 0-0 Prisons na Simba 2-0 Ndanda.
Ikishinda mbele ya Ndanda itafikisha pointi 86 ambazo hazitafikiwa na wapinzani wake wote, itasaliwa na mechi tano ambazo zitakuwa za kukamilisha ratiba na ikishinda mechi zote itafikisha jumla ya pointi 101.

Wapinzani wao, Yanga wana vigongo vikali 11 ambapo itakuwa ni mbele ya Mwadui itakayocheza nayo mara mbili, moja Taifa na ya pili Uwanja wa Kambarage kutokana na msimu huu kutokutana, kisha itakutana na JKT (Jamhuri) ambapo mechi ya kwanza Yanga ilishinda mabao 3-2 (Uhuru).
Baada ya hapo, kazi itakuwa mbele ya Azam ambapo mchezo wa kwanza Yanga ilipoteza kwa bao 1-0 (Taifa), pia itakutana na Namungo baada ya awali kutoka sare ya 1-1 (Taifa).
Ndanda itashuka Taifa ikiwa na kumbukumbu ya kufungwa bao 1-0 (Nangwanda), Biashara itaikaribisha Yanga (Karume), ambapo mchezo wa kwanza ilipoteza kwa kufungwa bao 1-0.
Yanga itaifuata Kagera Sugar, Kaitaba ambapo mechi ya kwanza jijini Dar, Kagera ilishinda mabao 3-0.
Yanga itarejea Bongo kucheza na Singida United (Taifa) na kwenye mchezo wao wa kwanza Yanga ilishinda 3-1, kisha itapambana na Mtibwa iliyokubali kichapo cha bao 1-0 (Jamhuri) mwisho ni dhidi ya Lipuli (Samora) iliyopoteza kwa kufungwa mabao 2-1 ilipokuja Dar.
Upande wa Azam FC, wao mechi zao zilizobaki ni mbele ya Mbao, Yanga (zote Taifa), Kagera (Kaitaba), Biashara (Karume), Singida, Mwadui (zote Taifa), Mtibwa (Gairo), Lipuli (Samora), Mbeya City na Prisons zote itakuwa Uwanja wa Sokoine.

Matokeo yao ya mechi za kwanza yalikuwa hivi;
Azam 1-0 Yanga, Azam 0-0 Kagera, Azam 2-1 Biashara United, Singida United 1-2 Azam, Mwadui 0-1 Azam, Azam 2-0 Mtibwa, Azam 2-0 Lipuli, Mbeya City 1-1 Azam na Azam 1-1 Prisons.

Yanga na Azam zikishinda mechi zao zote zilizosalia, zitafikisha pointi 84 kila mmoja, hivyo haziwezi kuifikia Simba kama ikishinda mechi tano tu.
SOMA NA HII  MUONEKANO WA UKURASA WA MBELE GAZETI LA SPOTI XTRA ALHAMISI