Home Uncategorized KWA LUC EYMAEL, YAGA WACHUKUE UAMUZI HUU HARAKA….

KWA LUC EYMAEL, YAGA WACHUKUE UAMUZI HUU HARAKA….




NA SALEH ALLY
YANGA walianza msimu vizuri wakionekana kuwa ni washindani wakubwa wa Simba na Azam FC na ilionekana kama si ubingwa uhakika ni nafasi ya pili.

Kawaida Azam FC, Simba na Yanga ndio timu zinazopewa nafasi ya kufanya vizuri zaidi katika Ligi Kuu Bara kwa takribani kila msimu.

Timu ambayo inaweza kufanya vema dhidi ya timu hizo, maana yake inakuwa na ubora na nafasi ya kuwa zile zinazomaliza katika nafasi za juu.

Wakati Yanga inakwenda kumalizia msimu, hata nafasi ya pili ilionekana ni kitu kigumu hata kupata nafasi ya pili tu katika Ligi Kuu Bara.

Yanga imekuwa ikipambana na nafasi hiyo dhidi ya Azam FC kwa kuwa Simba tayari ilishabeba ubingwa mapema sana ikiwa imeizidi Yanga kwa zaidi ya pointi 15.

Hii maana yake, Simba ilionyesha kuwa iko katika anga tofauti, bila ya ubishi ni kusema si saizi ya Yanga ambayo ilionekana mwanzoni kwamba ina kila uwezo wa kushindana nayo.

Kwa sasa unaona, Mkuu wa benchi la ufundi la Yanga, Luc Eymael ndiye mtu sahihi kwa wakati hii ambaye anaweza kubadilisha mambo kwa kushirikiana na uongozi wa klabu hiyo kuleta mabadiliko.
Wakati huu ndio mwafaka kwa kuwa msimu ndio umeisha jana rasmi lakini kama unavyojua kuwa msimu ujao utaanza mapema sana kwa kuwa kulikuwa na mabadiliko ya msimu kutokana na Covid 19 iliyolazimisha ligi mbalimbali na michezo duniani kusimama.

Kwa kuwa hali iko hivyo kwa sasa ni muda ambao Yanga wanataka kusajili kwa kuanza kubadilisha kikosi chao kwa kuangalia makosa yao na upungufu ambao wanaamini uliwafanya wakatoka relini hatua za mwisho.

Ambaye anapaswa kuwa mshauri namba moja kupitia ripoti ya mwisho wa msimu ni Eymael kwa kuwa ndiye amemaliza msimu na Yanga. Hii maana yake, kwa sasa kunatakiwa kuwa na ukaribu mkubwa sana kati ya Yanga na bosi huyo.

Kawaida ripoti yake itatumika kuyafanyia kazi yote yaliyoonekana kama ni upungufu. Lakini kama atakuwepo, mambo yanaweza pia kuwa rahisi sana kwa kuwa atakuwa akitoa ushauri kuhakikisha kikosi kinaimalika kwa ajili ya msimu ujao kwa kuwa utaanza mapema kuliko ilivyo kawada.

Swali la kujiuliza ni hivi; je, Yanga na Eymael wako vizuri? Kwa kuwa hawa wawili wanapaswa kuungana na kufanya kazi kwa ukaribu kwa ajili ya kukiunganisha kikosi chao.

Hawa wawili, kama watakuwa na tofauti sasa, wanaweza wakatengeneza ufa kwa msimu mzima ujao kwa kuwa hawatakuwa wameungana katika wakati huu mwafaka wa kurekebisha mambo yaliyowasumbua msimu uliopita.

Nilimsikia mara kadhaa Eymael akililala, akionyesha kuwa kuna mambo hakubaliani nayo hadi kufikia kuona kama anahujumiwa. Hadi anafikia kutoa hisia zake namna hii maana yake kuna jambo ambalo halimfurahishi.

Kama lipo, basi yanga wafanye hivyo, wakae na kuhakikisha wanalimaliza ili kutengeneza utulivu kwa kocha huyo aweze kuyafanya majukumu yake vizuri.

Itapendeza sana kama Eymael anakitengeneza kikosi chake, basi awe anajua atakuwepo nay eye ndiye atakuwa mhusika mkuu kama kikosi hakitafanya kazi tena katika msimu uhao wa Ligi Kuu Bara na michuaho mingine.

Kama Yanga inaona inahitaji mabadiliko katika benchi la ufundi, basi iwe sasa. Ninamaanisha hivi, kama wanaona wanahitaji kocha mpya au mbadala wa Eymael, basi wamuambie mapema ili aweze kwenda na kama yupo mteule anayechukua nafasi yake, basi apewe hiyo nafasi na kumalizana naye mapema ili aweze kuifanya kazi yake pia.

Muda ni mchache, kama Eymael yupo, apewe ushirikiano kama anaondoka, nayo iwe mapema, aende zake na anayekuja aanze kazi.






SOMA NA HII  KIKOSI CHA TIMU YA TAIFA YA BURUNDI KITAKACHOWASILI KESHO BONGO KWA AJILI YA MECHI DHIDI YA STARS