Home Uncategorized MSERBIA WA YANGA AKABIDHIWA MAFAILI YA KAGERA SUGAR

MSERBIA WA YANGA AKABIDHIWA MAFAILI YA KAGERA SUGAR


 KOCHA Mkuu wa Yanga, Mserbia, Zlatko Krmpotic amesema amepokea faili zote za Kagera Sugar ambao wanapambana nao leo hivyo anaindaa timu yake kuhakikisha inawatesa wapinzani wake.

 

Kagera atakuwa mwenyeji wa Yanga kwenye Uwanja wa Kaitaba leo ambapo mpaka sasa rekodi zinaonyesha katika mechi 20 walizokutana kuanzia msimu wa 2010/11 Yanga imeshinda mara 16 na Kagera mara nne.


Na msimu huu katika mechi mbili ambazo kila moja imecheza Yanga imeshinda moja na sare moja, wakati Kagera wametoka sare moja na kupoteza moja.

 

Akizungumza na Championi Jumamosi, Mserbia huyo alisema kuwa tayari uongozi wa Yanga ulimkabidhi mafaili yanayoihusu Kagera Sugar mapema tu jambo ambalo limemfanya kuandaa mfumo maalum ambao anaamini utaisaidia Yanga kuibuka na ushindi mnono leo.


“Nimekabidhiwa kila kitu kuhusu Kagera Sugar, kwa upande wangu nitakuwa muongo kusema nilikuwa naifahamu Kagera ila tayari viongozi wamenisaidia kuifahamu ni timu ya aina gani jambo ambalo tayari nishalifanyia kazi kwa kuwapatia mbinu mbalimbali wachezaji wangu ambao naamini kwa kiasi kikubwa zitatusaidia kupata ushindi.

 

“Kuhusu wachezaji wangu naona kuna maelewano mazuri kuliko ilivyokuwa awali, kadri siku zinavyozidi kwenda na maelewano yanazidi kuongezeka, ndio maana utaona niliomba mchezo wa kirafiki dhidi ya Mlandege ili kuongeza maelewano ya wachezaji wangu kwa kuwa naamini kupitia michezo mingi ndipo maelewano yanapoongezeka,” alisema kocha huyo.


Wakati huohuo, Mkurugenzi wa Uwekezaji wa GSM, Injinia Hersi Said, aliongeza kwa kusema: “Naliamini benchi la ufundi likiongozwa na kocha mkuu pamoja na wachezaji ambao kwa kiasi kikubwa naamini watatupatia ushindi mzuri kuelekea mchezo wetu mwingine wa ligi dhidi ya Kagera Sugar.

 

”Yanga baada ya kucheza michezo miwili ya ligi kuu imevuna pointi nne baada ya kutoa sare mchezo wake wa kwanza wa ligi dhidi ya Tanzania Prisons 1-1, kisha kupata ushindi katika mchezo wake wa pili dhidi ya Mbeya City kwa bao 1-0.

SOMA NA HII  KILICHOMCHIMBISHA HITIMANA THIERY NDANI YA NAMUGO CHATAJWA