Home Azam FC AZAM FC :MECHI ZA YANGA NA SIMBA NI PRESHA,ILA HATUNA HOFU

AZAM FC :MECHI ZA YANGA NA SIMBA NI PRESHA,ILA HATUNA HOFU

 GEORGE Lwandamina,  Kocha Mkuu wa Azam FC amesema kuwa mchezo wao wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Simba utakuwa na presha kubwa ila ataingia uwanjani kama mechi za kawaida.

Lwandamina ambaye alichukua mikoba ya Aristica Cioaba ambaye alifutwa kazi siku moja baada ya kuboronga mbele ya timu ya Yanga amesema kuwa anatambua haitakuwa kazi nyepesi kuvaana na Simba.

Cioaba alifutwa kazi baada ya vinara wa Ligi Kuu Bara wakiwa na pointi 44 kumnyoosha kwa bao 1-0 kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara uliochezwa Uwanja wa Azam Complex na mabosi wa timu hiyo waliweka wazi kuwa hakuwa na mwendo mzuri ndani ya timu.

Februari 7, Lwandamina atakuwa na kazi ya kusaka pointi tatu muhimu mbele ya Simba inayonolewa na Kocha Mkuu,  Didier Gomes ambaye amerithi mikoba ya Sven Vandenbroeck ambaye yupo ndani ya timu ya FAR Rabat.

Lwandamina amesema:-“Utakuwa mchezo mgumu ila tupo tayari kwa ajili ya ushindani na ninajua kwamba kila mmoja anafikiria juu ya presha hilo lipo wazi ikiwa unacheza na Simba ama Yanga.

“Ni mchezo wa kawaida hivyo tutaingia ndani ya Uwanja kwa kujiamini na kujituma zaidi ili kupata ushindi,”.

Azam FC ipo nafasi ya tatu na pointi 32 baada ya kucheza mechi 17 inakutana na Simba iliyo nafasi ya pili na pointi 35.

SOMA NA HII  AZAM FC MIKONONI MWA WAMISRI KIMATAIFA