Home Ligi Kuu DODOMA JIJI WAIPIGA MKWARA SIMBA, NGOMA NI JAMHURI,DODOMA

DODOMA JIJI WAIPIGA MKWARA SIMBA, NGOMA NI JAMHURI,DODOMA


 MBWANA Makata, Kocha Mkuu wa Dodoma Jiji amesema kuwa kikosi chake kipo tayari kwa ajili ya mchezo wa kesho wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Simba na ataingia uwanjani kwa kujiamini kusaka pointi tatu.

Mchezo wa kesho ni kiporo cha mzunguko wa kwanza kwa Dodoma Jiji na Simba kutokana na wageni Simba kuwa na ratiba kwenye mechi za Ligi ya Mabingwa Afrika.

Kesho Dodoma Jiji itawakaribisha Simba, Uwanja wa Jamhuri Dodoma majira ya saa 10:00 jioni kwa timu zote kusaka pointi tatu muhimu.

Unatarajiwa kuwa mchezo mgumu na wenye ushindani kutokana na rekodi za Dodoma Jiji ikiwa nyumbani kuwa ngumu kuyeyusha pointi huku Simba ikiwa inahitaji kutetea taji lake la Ligi Kuu Bara pamoja na kupunguza mzigo wa pointi ambazo kinara wa Ligi Kuu Bara anazo.

Dodoma Jiji ipo nafasi ya 10 baada ya kucheza mechi 17 kibindoni ina jumla ya pointi 22 inakutana na Simba iliyo nafasi ya pili na kibindoni ina pointi 35 baada ya kucheza mechi 15.

Kinara Yanga ana jumla ya pointi 44 baada ya kucheza jumla ya mechi 18 hivyo amemuacha Simba kwa pointi 9 ikiwa itapoteza itaongeza mzigo na ikishinda itapunguza hata ikiambulia sare pia itapunguza pointi.

Makata amesema:”Tupo kamili kwa ajili ya mchezo wetu, tutaingia kwa tahadhari kubwa kuona namna gani tutapata matokeo.

“Tunawaheshimu wapinzani wetu hilo lipo wazi ila nasi tunahitaji pointi tatu,” .

Pia uongozi umeweka wazi kuwa mchezo wa kesho Februari 4 utachezwa Jamhuri, Dodoma na sio Jamhuri, Morogoro kama ambavyo wengine wamekuwa wakieleza.

SOMA NA HII  HIZI HAPA LEO ZA LIGI KUU BARA ZITACHEZWA