Home Yanga SC EYMAEL: KUIFUNGA SIMBA MBELE YA JPM NI KUMBUKUMBU KWANGU NA WACHEZAJI

EYMAEL: KUIFUNGA SIMBA MBELE YA JPM NI KUMBUKUMBU KWANGU NA WACHEZAJI


 LUC Eymael, aliyekuwa Kocha Mkuu wa Yanga msimu wa 2019/20 amesema kuwa moja ya kitu ambacho anakikumbuka muda wote ni ushindi wake mbele ya Simba kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara uliochezwa Uwanja wa Mkapa.

Mchezo huo ulichezwa Uwanja wa Mkapa, Machi 8,2020 na baada ya dakika 90 ubao ulisoma Yanga 1-0 Simba.

Bao pekee ambalo alilishuhudia pia aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Pombe Magufuli lilipachikwa kimiani na Bernard Morrison na kuwafanya Simba wayeyushe pointi tatu.


Kwa sasa baada ya Magufuli kutangulia mbele za haki Machi 17,2021 Samia Suluhu ni Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa katiba ambapo awali alikuwa ni makamu wa JPM. Leo Machi 30, Samia amemchagua Philip Mpango awe Makamu wa Rais wa Tanzania ambapo jina lake limepitishwa na Wabunge kwa asilimia 100.

Eymael ambaye kwa sasa yupo Ubelgiji amesema kuwa anakumbuka mchezo huo kwa namna ambavyo Magufuli aliweza kuhudhuria na timu yake ilishinda jambo ambalo halifutiki kwake.

“Nakumbuka kwamba nilipokuwa nikifundisha Yanga niliwafunga Simba mbele ya Rais JPM, alikuwa ni kiongozi shupavu na mpenda haki kwa kuwa ametangulia mbele za haki hakuna namna ninamuombea apumzike kwa amani.

“Ushindi wetu mbele yake ilikuwa ni furaha hivyo bado itabaki kuwa alama kwangu pamoja na wachezaji ambao walianza siku hiyo, na kwenye maisha yangu ya kazi Tanzania ule ni mchezo ambao nilipenda kiwango cha wachezaji wangu.

“Pia unabaki kwenye kumbukumbu yangu pamoja na wachezaji kiujumla. Nilishangaa namna ambavyo walicheza kwa juhudi bila kuchoka,” .

Kwa sasa Morrison ni mchezaji wa Simba inayonolewa na Kocha Mkuu, Didier Gomes.

SOMA NA HII  KAMA ULIKUWA HUJUI...YANGA NA NABI WADAIWA DENI HILI LA CAF...LAZIMA LILIPWE LEO...LA SIVYO SIMBA ITAENDELEA KUWA JUU...