Home Simba SC KUHUSU KUKAA BENCHI..KAGERE AVUNJA UKIMYA SIMBA

KUHUSU KUKAA BENCHI..KAGERE AVUNJA UKIMYA SIMBA


HUKO mitaani na hata kwenye mitandao ya kijamii kumekuwa na maneno mengi juu ya kupigwa benchi mfululizo kwa straika Meddie Kagere, lakini mwenyewe ameamua kuvunja ukimya, huku Kocha Mkuu wake, Didier Gomes alifunguka kila kitu, akiwataka mashabiki wa Simba watulie.

Kagere anayeshikilia rekodi ya kuwa Mfungaji Bora misimu miwili mfululizo 2018-2019 na 2019-2020, tangu kuanza kwa msimu huu amekuwa hapati nafasi ndani ya kikosi cha kwanza tofauti na misimu hiyo miwili ya nyuma.

Mnyarwanda huyo mwenye asili ya Uganda, alianza kusota benchi tangu Simba ikiwa chini ya Kocha Sven Vandenbroeck aliyetimkia FAR Rabat ya Morocco, lakini alipokuja Gomes alianza kupata nafasi kikosi cha kwanza kabla ya kurejeshwa tena benchi na kuzua maneno.

Hata hivyo, akizungumza juzi, Kagere alisema kukaa kwake benchi wala hakumpi presha kwani anaamini bado ni mshambuliaji mzuri mwenye kiwango, isipokuwa kila kocha huwa na chaguo lake.

Kagere alisema amekuwa akiona na kusikia maneno kutoka sehemu tofauti juu ya kutopangwa kwake, lakini yeye kama mhusika analichukua hilo kama changamoto na anaendelea kuamini ni suala la muda tu kabla naye kupewa nafasi na Kocha Gomes kikosini.

“Sijashuka kiwango, nipo kama nilivyokuwa awali kipindi natumika kikosi cha kwanza, ninaendelaa kujifua kama kawaida, kwani najua hata nikipewa nafasi napaswa kuonyesha uwezo huo,” alisema Kagere na kuongeza;

“Unajua kila kocha huwa na wachezaji wake anaotaka kuwatumia kulingana na mechi husika na jambo hilo ndio nakutana nalo kwa kutumika kama mbadala na kuna ambaye anaanza katika kikosi cha kwanza.”

Lakini alisema licha ya kuwekwa benchi, hajajiachia kama mtu aliyekaa tamaa, kwani huwa hana utamaduni wa kukata tamaa isipokuwa anajua ni upepo tu unapita na atarejea kwenye nafasi yake kikosini.

Alisema kama akipata nafasi ya kucheza japo kwa dakika chache katika mechi au asipotumika kabisa huwa anatenga muda ule ule ambao utakuwa sawa na dakika 90, za mechi ambazo alitakiwa kucheza ili kufanya mazoezi ya nguvu.

SOMA NA HII  ACHANA NA SHABAN CHILUNDA MWAMBA MWINGINE HUYU HAPA KATUA MSIMBAZI

“Nina imani mazoezi haya ya nguvu ambayo nayafanya kama nikiwa sijacheza nakuwa nimetumika kama wale wenzangu waliocheza ili kuwa sawa na sijawahi kuona naonewa au kuongea kokote zaidi ya kujiandaa ili nikipewa nafasi niweze kuonyesha ubora,” alisema Kagere na kuongeza;

“Sitamani kuona kazi yangu kisoka inakwenda chini kirahisi nitapambana na nitacheza kama ilivyokuwa hapo awali, lakini kuhusu suala la kufunga hilo huwa linatokea kama nikipata nafasi ya kucheza mara kwa mara.

“Ukiangalia licha ya kucheza mechi chache bado nipo kileleni mwa ufungaji wa mabao katika ligi msimu huu na bado nina nafasi ya kuongeza, hivyo nahitaji yangu katika mechi yakifika nina imani nitapewa nafasi,” alisisitiza Kagere aliye na mabao tisa kama nahodha wake, John Bocco.

Naye Kocha Gomes alisema kikosi chake kina wachezaji 30 na wote wapo katika viwango bora na kila ambaye amekuwa akimpatia nafasi ya kucheza amekuwa akionyesha ubora wake katika kutimiza majukumu na sio kama Kagere hana nafasi kwake.