Home Azam FC AZAM FC KAMILI GADO KUMALIZANA NA WASOMALIA LEO, KILA LA KHERI

AZAM FC KAMILI GADO KUMALIZANA NA WASOMALIA LEO, KILA LA KHERI


 HOMA ya jiji kwa sasa ni juu ya mchezo wa kibabe kwa wawakilishi wa Tanzania katika Kombe la Shirikisho ambao unawahusu Azam FC dhidi ya Horseed FC ya kutoka Somalia.


Mchezo huo unatarajiwa kuchezwa leo Septemba 11,saa 1:00 usiku ni pale Uwanja wa Azam Complex ambapo hii ni kete ya kwanza kwa wawakilishi wa Tanzania na kazi yao ni moja tu kusaka ushindi.


Licha ya kwamba Azam FC imeweza kufanya usajili mzuri ambao unawapa kiburi cha kutamba mtaani pamoja na kambi iliyokuwa nchini Zambia kwa muda, bado wawakilishi hawa wanapaswa wasiwachukulie poa wapinzani wao ikitoea hali hiyo basi watamalizwa kimyakimya kama sera yao inavyosema.


Pia Azam FC ina kazi ya kusaka ushindi kwa idadi kubwa ya mabao kwa kuwa mchezo wao wa pili watakuwa ugenini na soka la Afrika ni la kivyetuvyetu wakizembea basi picha linaweza kuisha mapema.


Wawakilishi hao wa Tanzania wapo kamili gado kwa ajili ya kupeperusha bendera kimataifa.


Wapinzani wao


Historia inaonyesha kwamba wapinzani wa Azam FC ni wakongwe kwa kuwa timu hiyo ilianzishwa mwaka 1971 nchini Somalia na wana mataji 8 ya Ligi Kuu ya Somalia hivyo bado ni timu inayohitaji nidhamu.


Timu hiyo inanolewa na Kocha Mkuu, Abdi Hamid Moallin ambaye anawanoa vijana hao wanaotumia Uwanja wa Banadir na una uwezo wa kubeba watazamaji 15,000.


Mataji yake iliyotwaa kwenye Ligi Kuu ya Somalia ilikuwa ni 1972,1973,1974,1977,1978,1980,2020/21 kwa upande wa Azam FC inayonolewa na Kocha Mkuu, George Lwandamina ina taji moja la Ligi Kuu Bara ilisepa nalo msimu wa 2013/14 na ilianzishwa mwaka 2004.


Hesabu za Azam FC


Azam FC kupitia kwa Mtendaji Mkuu wa timu hiyo, Abdulkalim Amin, iliweka wazi kuwa inahitaji kusona mbele kwenye Kombe la Shirikisho hivyo hiki ni kibarua kikubwa kwa wachezaji wao kusaka ushindi.


“Kwa kuwa tumeweza kupata nafasi ya kushiriki kwenye mashindano ya kimataifa ni lazima tupambane ili kufanya vizuri katika hatua za mwanzo kwa kupata matokeo mazuri.

SOMA NA HII  BANGALA SASA KUKIPIGA DHIDI YA YANGA AGOUST 9, CHEKI AKIJIFUA KAMBINI NA AZAM


“Kwanza tunataka kuanza kupita kwenye hii hatua ya awali na kufika hatua ya mtoano kisha baada ya hapo hesabu zetu kubwa ni kuona tunatinga hatua ya makundi.


“Haitakuwa kazi rahisi hasa ukizingatia kwamba haya ni mashindano ya kimataifa na kila timu inahitaji ushindi hivyo nasi pia tunahitaji kupata ushindi,” alisema Amin.


Kambi ya Zambia


Kambi ya muda ambayo iliwekwa na timu hiyo nchini Zambia pamoja na mechi za kirafiki za kimataifa zinatajwa kuwapa nguvu Azam FC kwa kuweza kupata kile ambacho wanakihitaji jambo ambalo linawapa nguvu kuelekea kwenye mchezo wa leo.


Kwa mujibu wa Kocha Msaidizi wa Azam FC, Vivier Bahati aliweka wazi kuwa kwa namna ambavyo wachezaji walikuwa wakipambana kwenye mazoezi pamoja na mechi kuna jambo litatokea.


“Wachezaji walikuwa kwenye kazi kubwa na maendeleo yao yamekuwa mazuri kila leo hivyo tunaamini kwamba tutapata matokeo chanya kwenye mechi zetu.


“Kikubwa ni kuona kwamba kile ambacho tumekifanyia kazi mazoezini kinaonekana uwanjani, “alisema Bahati.


Kila la kheri Azam FC tayari Biashara United wao biashara yao ugenini walimaliza kazi ni kwenu kusepa na ushindi licha ya mashabiki kutokuwepo ila kila kitu kinawezekana.