Home news ISHU YA NYOTA WATATU KUKOSEKANA MBELE YA WANAIJERIA YANGA YASEMA NI PENGO

ISHU YA NYOTA WATATU KUKOSEKANA MBELE YA WANAIJERIA YANGA YASEMA NI PENGO


 UONGOZI wa Yanga umeweka wazi kuwa kuwakosa nyota wao watatu kwenye mchezo wao wa kimataifa dhidi ya Rivers United ni pengo kwa kuwa hao ni wachezaji muhimu.

Kuna uwezekano mkubwa kwa mabingwa hao mara 27 wa Ligi Kuu Bara kukosa huduma za nyota wao wapya ambao ni Khalid Aucho ambaye ni kiungo, Fiston Mayele ambaye ni mshambuliaji pamoja na Shaban Djuma ambaye ni beki kutokana na kukosa hati ya Uhamisho ya Kimataifa, (ITC).

Ofisa Habari wa Yanga, Haji Manara amesema kuwa wanatambua umuhimu wa wachezaji hao na kukosekana kwao ni pengo kubwa jambo ambalo linawafanya wapambane ili kupata vibali vyao.

“Hawa ni wachezaji wetu wakubwa na kuwakosa kwenye mechi zetu ni pengo kubwa hivyo lazima tupambane ili kuona namna gani tunaweza kuwa nao kwenye mechi zetu.

“Haina maana kwamba haya ni makosa ya Yanga, hapana sisi tuliweza kujitahidi na kufuata utaratibu kwa wakati ila tatizo ilikuwa kwa timu ambazo walitoka wachezaji hao kushindwa kutoa vibali kwa wakati.

“Bado tuna nafasi ya kufanya vizuri kwani wachezaji wapo wengi ndani ya Yanga na ndio maana tukaitwa Yanga, sisi ni mabingwa wa muda wote tunaamini kwamba tutafanya vizuri, kikubwa mashabiki wawe nasi bega kwa bega,” amesema Manara.

Septemba 12, Yanga inatarajiwa kuwakaribisha River United kwenye mchezo wa awali wa Ligi ya Mabingwa unaotarajiwa kuchezwa Uwanja wa Mkapa.

SOMA NA HII  NJAA YAIFANYA NDANDA FC KUWA KAMA CHELSEA AISEE...MABOSI WAAMUA KUIUZA BILA MASHARTI MENGI...