Home news MEDDIE KAGERE AFUNGA MABAO 59 BONGO

MEDDIE KAGERE AFUNGA MABAO 59 BONGO


MEDDIE Kagere mshambuliaji wa kwanza kutupia ndani ya kikosi cha Simba kwa msimu wa 2021/22 ndani ya Ligi Kuu Bara kwa sasa ameweza kufikisha jumla ya mabao 59 ndani ya ligi akiwa amecheza misimu mitatu kwa sasa.

Nyota huyo ambae aliibuka Simba msimu wa 2018/19 akitokea Klabu ya Gor Mahia amekuwa akitajwa kuwa moja ya washambuliaji hatari ila amekuwa akibezwa na mashabiki wakidai kwamba ni mzee jambo ambalo Kagere alisema kuwa hilo hajali yeye anafurahi kufanya kazi.

Kagere ambaye wengi hupenda kumuita MK 14 yupo ndani ya kikosi hicho cha Simba ambacho kwa sasa kinapambana kuweza kutetea taji la Ligi Kuu Bara ambalo walitwaa msimu uliopita wa 2020/21.

Msimu wake wa kwanza alitupia mabao 23 na alikuwa ni mchezaji wa kwanza kufunga bao ndani ya Simba alifunga bao hilo Uwanja wa Mkapa mbele ya Tanzania Prisons na Simba ilimaliza msimu huo kwa kufunga jumla ya mabao 77 baada ya kucheza mechi 38.

Pia kwa msimu huo aliweza kunyanyua mikono kwa kuwa Simba ilisepa na taji pia la ligi na kuwa miongoni mwa maingizo mapya yaliyoweza kutwaa taji hilo kubwa Bongo.

Msimu wa 2019/20 Kagere alitupia jumla ya mabao 22 na alikuwa ni namba moja kwa utupiaji pia alikuwa mchezaji wa kwanza Simba kufunga ambapo alifunga bao la kwanza mbele ya JKT Tanzania, Uwanja wa Uhuru.

Hata msimu huo pia Simba ilisepa na taji la Ligi Kuu Bara na kuweza kuendelea pale ambapo iliishia msimu uliopita.

Msimu wa 2020/21 Kagere alitupia mabao 13 alikuwa ni namba tatu kwa utupiaji na namba moja alikuwa ni John Bocco ambaye alifunga mabao 16 na pasi mbili za mabao.

 Kwa msimu wa 2020/21 mfungaji wa bao la kwanza ndani ya kikosi cha Simba alikuwa ni nahodha Bocco aliyefunga bao lake la kwanza mbele ya Ihefu FC wakati Simba ikishinda mabao 2-1.

Msimu huu wa 2021/22 Kagere amekuwa mchezaji wa kwanza kufunga ndani ya Simba ilikuwa mbele ya Dodoma Jiji dakika ya 69 akitokea benchi na kuipa pointi tatu timu yake inayonolewa na Kocha Mkuu, Didier Gomes.

SOMA NA HII  BAADA YA NGAO YA JAMII NGUVU YA YANGA IPO HUKU

Ulikuwa ni ushindi wa kwanza kwa Simba kwa msimu wa 2021/22 kwa sababu katika mechi zake ilizocheza hivi karibuni ilikwama kushinda.

Kuanzia ule mchezo wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya TP Mazembe ilinyooshwa bao 1-0 Uwanja wa Mkapa na ule wa Ngao ya Jamii dhidi ya Yanga ilionjeshwa joto ya jiwe kwa kufungwa bao 1-0 na mchezo wa kwanza wa ligi ililazimisha sare ya bila kufungana na Biashara United.

Imeandikwa na Dizo_Click