Home news ‘BATGOL’ : KWA SIMBA HII…ATAPIGWA MTU MPAKA ACHAKAE…AGUSIA UBUTU WA KAGERE NA...

‘BATGOL’ : KWA SIMBA HII…ATAPIGWA MTU MPAKA ACHAKAE…AGUSIA UBUTU WA KAGERE NA BOCCO…


TRAIKA wa zamani wa Simba, Emmanuel Gabriel ‘Batgol’ amekiangalia kikosi cha sasa cha Simba na kusema sio kibaya kama watu wanavyosema na kuikingia kifua safu ya ushambuliaji ya timu hiyo inayoongozwa na John Bocco na Meddie Kagere akidai wala sio butu licha ya kasi ndogo ya ufungaji.

Batgol alisema mashabiki wanaoiponda Simba kwa sasa ni kwa sababu walizoeshwa kuona ikitoa dozi nene kitu ambacho katika mechi nne zilizopita haijafanya na kudai kadri ligi itakavyochangamka kuna mtu atapigwa nyingi uwanjani na kushindwa kuamini kama ni Simba hii hii.

Akizungumza hivi karibuni, Batgol alisema Simba ilizoea kutembeza vipigo vikubwa kwa wapinzani wake lakini safari hii timu zimeimarika zikiwa na nguvu ya fedha na vikosi hivyo sio rahisi kufungwa kiwepesi, lakini bado anaamini Simba itakuja kushangaza watu mbele ya safari.

Nyota huyo aliyedumu Msimbazi kwa miaka nane alisema bado washambuliaji wa Simba wanaweza kufanya mambo makubwa na kuisaidia timu yao msimu huu.

“Hakuna kilichobadilika Simba, sema tu ligi imekuwa ngumu ushindani umeongezeka, walizoea pasi 100 wanafunga mabao lakini sasa timu hazitaki kupoteza pointi kirahisi, ndio maana unaona timu zinafungwa zinahuzunika,” alisema Batgol.

“Sio kwamba forward (washambuliaji) ni butu bali hali tu imebadilika, lakini huko mbele ya safari kuna watu watapigwa nyingi na kushindwa kuamini, Simba inatengeneza timu baada ya watu waliokuwa wakiichezesha kuondoka kwa mpigo, lakini mjue kila timu inahitaji matokeo mazuri.”

Aidha Batgol ambaye kwa sasa ni Meneja wa Mbeya Kwanza aliwapigia chapuo wachezaji wa kikosi chake akiwamo William Edward, Oscar Mwajanga, Khamis Kanduru, Paul Peter na Crispin Ngushi kuitwa timu za taifa za vijana na wakubwa kwani wana uwezo mkubwa unaoweza kulisaidia taifa.

“Wachezaji wengi wamefanya vizuri katika hizi mechi tano za mwanzo nawapongeza vijana wangu ni wadogo wanapambana watoke licha ya ugeni wao kwenye ligi, kwa kweli tunajivunia kuwa nao hapa na hawa kina William na Ngushi wakipata nafasi wanaweza kuibeba taifa wakipewa nafasi,” alisema.

SOMA NA HII  KIFAA KIPYA YANGA CHAANZA NA MKWARA WA KUFA MTU...AJITOFAUTISHA NA WENZAKE...