Home CAF KISA UBINGWA WA LIGI..MASTAA YANGA WAPEWA MASHARTI MAPYA…WAKATAZWA KUFANYA MAPENZI…

KISA UBINGWA WA LIGI..MASTAA YANGA WAPEWA MASHARTI MAPYA…WAKATAZWA KUFANYA MAPENZI…


KWENYE mahojiano ya kocha wa mazoezi ya viungo wa Yanga, Helmy Gueldich  alielezea mambo mbalimbali na baada ya kuangalia jinsi alivyoanza kazi yake ndani ya timu hiyo sasa anaendelea kuelezea rekodi za ubora wa wachezaji wake.

Kwenye mahojiano maalumu na Gazeti la  Mwanaspoti Jijini Dar es Salaam, Helmy ameweka wazi baadhi ya masharti mapya aliyowapa mastaa wa timu hiyo ili wakae sawa na waendane na kasi inayotakiwa msimu huu ambayo itarejesha makombe Yanga.

Helmy anaeleza kitu kikubwa cha kwanza ni kuzingatia muda wa kupumzika na wakati wa kupumzika wanatakiwa kuhakikisha wanapata mapumziko kamili na si kufanya mambo mengine ambayo yatawazuia kuendana na kasi ya mazoezi au programu za ndani na nje ya Uwanja.

“Kitu kimoja ambacho anapenda kusema Kocha Jose Mourinho kitu muhimu kwa mchezaji katika kupumzika ni akili yake kupumzika vizuri haitakiwi wakati wa kupumzika unafanya vitu vingine kwa hiyo hapa Yanga huwa tunafanya kazi kubwa mazoezini na nimewaambia wachezaji wanapotakiwa kupumzika wapumzike sawa sawa na kuuacha mwili uakisi kile kinachotakiwa,” anasema Helmy.

“Kitu kibaya zaidi ambacho nimewaambia hakitakiwi ni kunywa pombe. Kwangu mimi hii ndio mbaya zaidi nimewaambia sipendi kuona mchezaji anakunywa pombe nashukuru kwa wachezaji wote tulionao wanaheshimu hilo huwa tuna programu za kuwaondolea uchovu wachezaji baada ya kufanya kazi kubwa, tunatumia bwawa la kuogelea na mapipa ya barafu kama dakika tano halafu baadae unawaweka katika maji ya moto kidogo ili kuondoa sumu kwenye misuli ili damu ikimbie vizuri.

“Kingine kibaya ni uvutaji lakini sijaona kama kuna mchezaji hapa kwetu anavuta sigara na bahati nzuri huku Tanzania kuna joto tofauti na kule kwetu pia kuna suala la mchezaji kupenda kufanya mapenzi, nalo sijaona kama tatizo sana kwa kuwa bahati kubwa hapa Tanzania muda mrefu wachezaji wako kambini hivyo kama ni siku zile za mapumziko sio mbaya unajua wachezaji nao ni binadamu hatuwezi kuwafanya kama wafungwa.”

AMEOMBA KUPEWA HIVI;

“Bado kuna vitu ambavyo tumewaomba uongozi kutuletea ili tuongeze ubora wa wachezaji kuna vitamini ambazo wachezaji wanatakiwa kupewa nazo zitakuja kutusaidia lakini pia kuna vifaa maalum vya kupima uwezo wa mchezaji kukimbia (GPS) nazo zinakuja tutakuwa tunatumia kwa kila mchezaji kujua anavyocheza kama amefanya kazi kwa ubora wake au amepanda.

ANAWASILIANA NA WAZITO

Katika kuonyesha jamaa ana watu, kumbe huwa anawalisiliana na makocha wa viungo wa klabu za Bayern Munchen na Atletico Madrid ambao wanampa mbinu mbalimbali za kuwaongezea ubora wachezaji wa Yanga.

“Nina marafiki wengi lakini huwa napenda kujifunza kwa watu waliotuzidi, katika masomo yangu nilipata nafasi ya kufundishwa na makocha wakubwa wa mazoezi ya viungo Holger Broich wa Bayern Munchen na Oscar Ortega wa Atletico Madrid yalikuwa ni mafunzo mafupi.

SOMA NA HII  CAF WAPANGA 'MAPROO' BONGO KUKIPIGA DHIDI YA TAIFA STARS...MCHONGO MZIMA UKO HIVI...

“Duniani hawa ndio makocha ghali wa mazoezi ya viungo ambao wamesomea kazi hii mpaka kiwango cha udaktari usishangae ubora wa hizi klabu katika soka la wachezaji kukaba sana inatokana na kazi ya hawa watu.

“Huwa nawasiliana nao sana walifurahi kusikia nipo Tanzania wakataka kujua maendeleo yangu na huwa nawatumia kila programu kubwa zinazofinya kwa wachezaji na wamekuwa wakinipongeza na kuniongezea vitu zaidi ambavyo vimekuwa vikiwaongezea ubora wachezaji hapa Yanga.”

VYAKULA, SODA MARUFUKU

“Kambini bado tunataka kutengeneza pia mfumo mzuri wa chakula lakini kikubwa wachezaji wanapata juisi nzuri ya matunda na maji ya kutosha unajua hawa ni wachezaji wanatakiwa kupata maji kwa wingi kuweza kurudisha mwili katika utulivu na kuna chakula kizuri nawapongeza viongozi kwa kupambana katika hili.

“Unajua lazima tuseme kwa kambi hii ya Yanga kila kitu kinakuwa kinakwenda vizuri huku kuna utulivu mkubwa hata nyumba za wachezaji ziko mbali na barabara kubwa, haya ndio mazingira ambayo yanamfanya mchezaji kuwa bora nafahamu ni gharama lakini unapotaka matokeo bora unahitaji mazingira ya namna hii narudia nawapongeza sana uongozi wa klabu na wadhamini GSM ni kweli wameamua kufanya uwekezaji katika timu.”

WACHEZAJI GETI KALI

Kuna msemo wa mtaani watu wakiona nyumba yenye ulinzi mkali basi husema huyu mtoto ni geti kali, hapa tunaweza kusema pia wachezaji wa Yanga hili wanalo, Helmy anasema ni vigumu kwa mchezaji wa timu hiyo kutoroka kambini.

“Ukiwa mchezaji hupendi maisha ya kukaa kambini sana lakini kama kuna watu wanaumia basi ni wachezaji wa Yanga huku ukiingia kambini inajulikana mchezaji flani ameingia muda flani ndani kitu ambacho kinawakera ni hiki wakiwa huku hakuna mtu ambaye anavuka geti kutoka labda awe anatoka kwenda hospitali na hapo atakuwa na daktari au kama timu inakwenda kwenye programu.

“Huwa nawaona wanachukia sana kutokana na ulinzi wa hii kambi lakini kwetu kama makocha tunafurahi kwa kuwa tunaamini wachezaji wako katika ubora kama walivyokuwa jana.”

Tofauti soka la Tunisia na Bongo

“Hapa Tanzania watu wanapenda soka lakini bado hakuna uwekezaji mkubwa ambao unatakiwa kufanyika katika kuhakikisha yanapatikana matokeo bora, naweza kukupa mfano kule kwetu Tunisia sio kitu kigeni kuona kuna kocha wa viungo anatokea Hispania, Italia au Ubelgiji kwa kuwa waliamua kutaka mafanikio na sasa imekuwa kama utamaduni.

“Kule Tunisia kuanzia timu ya vijana ile ya watoto wadogo kabisa inakuwa na kocha mkuu, msaidizi, kocha wa makipa na kocha wa mazoezi ya viungo na madaktari hiyo inakwenda hadi timu kubwa lakini hapa Tanzania nimeshangaa watu kama mimi unawakuta klabu kubwa tu Yanga, Simba, Azam klabu zingine hazina hatua ya mabadiliko makubwa inaanzia hapo nafikiri klabu zinatakiwa kubadilika.”

Credit: Makala haya yameandikwa na kuchapishwa kwanza na wavuti la Mwanaspoti