Home news HIVI NDIVYO YANGA YA GSM ILIVYOIBOMOA SIMBA YA MO DEWJI KILAANI…MANARA NA...

HIVI NDIVYO YANGA YA GSM ILIVYOIBOMOA SIMBA YA MO DEWJI KILAANI…MANARA NA SENZO WATAJWA …


Simba Sc na Yanga ndio wababe na mabingwa wa nchi hii kwa miaka mingi sana kwenye michuano mbalimbali ikiwa ni pamoja na ligi kuu Tanzania bara, Mapinduzi Cup, Kagame Cup, ngao ya jamii pamoja na Azam Sports Federation Cup.

Moja ya vitu vya msingi vinavyopelekea Simba Sc na Yanga kushinda mataji haya ni pamoja na uwezo mkubwa wa fedha zinazotumika kuendesha timu zao, uwepo wa viongozi wazuri kwenye ngazi za juu za timu, uwepo wa watu bora kwenye benchi la ufundi la timu (makocha) pamoja na nguvu kubwa kutoka kwa mashabiki.

Ndani ya msimu miwili iliyopita klabu ya Yanga wameonekana kufanya jitihada kubwa ya kuhakikisha wanaweza mizizi ya ufalme wao kwenye ligi ili kuondoa ukubwa wa Simba Sc ambao wamekua wakitamba kwa kushinda mataji ligi kuu Tanzania bara kwa misimu minne mfululizo.

Yanga wametengeneza mazingira ya kuwavuta baadhi ya viongozi waliokua wanafanya kazi Simba Sc na kuwapa mikataba kwenye timu yao, mfano wa viongozi hao ni pamoja na Senzo Mbatha, Haji Sunday Manara pamoja na Milton Nienov.

GSM Na Jeuri Ya Fedha Ndani Ya Klabu ya Yanga

Klabu ya Yanga kwa sasa wameingia kwenye timu bora na kubwa nchini Tanzania kwa kua na uwezo wa kufanya mambo yao kwa wakati kwa kutegemea sana fedha ambazo zimewekwa na kampuni ya GSM ambao ndio wadhamini wakuu wa klabu ya Yanga.

Yanga wanafanya usajili wa wachezaji wakubwa, viongozi wakubwa na makocha wakubwa kutokana na hali nzuri ya kiuchumi iliyopo ndani ya klabu hiyo.

GSM mpaka sasa tunaweza kusema kwamba wamefanikiwa kubomoa kwa kiasi fulani ngome ya Simba Sc ambayo ilikua imara zaidi ndani ya misimu kadhaa iliyopita. GSM wamefanya mambo makubwa kwa kutoa mikataba minono kwa wachezaji wa klabu ya Yanga ambao wanaonyesha kiwango bora kwa sasa lakini pia wameongeza nguvu kubwa kwenye benchi la ufundi la klabu hiyo.

Nguvu Ya GSM Yahusishwa Kwenye Dili La Senzo Mbatha Kutoka Simba Sc na Kujiunga Na Yanga

Katika matukio makubwa ambayo yamewahi kutokea kwenye vilabu vya Simba Sc na Yanga miaka ya hivi karibuni ni pamoja na uhamisho wa mchezaji Bernard Morrison kutoka Yanga na kujiunga na Simba Sc, lakini pia uhamisho wa Senzo Mbatha kutoka Simba Sc na kuhamia Yanga ilikua ni habari ngumu sana.

Senzo ambaye kwa sasa anafanya kazi kama mtendaji mkuu wa klabu ya Yanga anatajwa kua mtu bora sana kwenye masuala ya maendeleo ya mpira. Senzo ameongeza kitu kikubwa sana ndani ya klabu ya Yanga kwa sasa na hakika GSM walifanya kitu bora sana kuhakikisha kwamba mtu huyu anashawishika na dili lao na kukubali kuachana na Simba Sc.

SOMA NA HII  MANARA: KUNA WATU WANATAKA KIKI KWA JINA LANGU...NILIPOFIKIA KIMAFANIKO WAO HATA NDOTONI HAWAJAFIKA...

Klabu ya Simba Sc walifanya jitihada za kupata mtu sahihi wa kubadili nafasi ya Senzo na walifanikiwa kumpata Barbara Gonzalez ambaye pia anafanya kazi nzuri ndani ya kikosi cha Simba Sc. Barbara Gonzalez amefanikiwa kuziba vizuri pengo la Senzo licha ya kwamba kuna vitu anavikosa kutokana na mahitaji ya kazi yake katika klabu ya Simba Sc tofauti na wakati ule ambao klabu ilikua chini ya Senzo Mbatha.

Manara Awashangaza Simba Sc Baada Ya Kukubali Kujiunga na Yanga

Uhamisho wa Manara kutoka katika klabu ya Simba Sc kwenda kujiunga na Yanga lilikua ni jambo la kushangaza sana lakini uhalisia umeendelea kudumu na kuona kwamba Manara ni mfanyakazi wa klabu ya Yanga na kwa kinywa chake mwenyewe alithibitisha kwamba amedumu kwenye klabu ya Simba Sc kutoka na mazingira ya kazi lakini moyo wake wote ulikua unapenda kuwashabikia Yanga Sc.

Manara alipokua anajiunga na klabu ya Yanga alitoa taarifa kwamba moja kati ya sababu zilizofanya akubaliane na ofa ya Yanga ni pamoja na kiasi kikubwa cha pesa ambazo aliwekewa mezani na GSM ikiwa ni sehemu ya makubaliano ya mkataba wake na matajiri hao. GSM amefanya ushawishi mkubwa sana kupata saini ya Manara na katika hili wanastahili pongezi nyingi sana.

Klabu ya Simba Sc pia wamefanya jitihada za kupata mtu sahihi ambaye anaweza kuongoza kitengo cha habari kwa umakini ambapo walifikia makubaliano ya kuingia mkataba na Ahmed Ally siku chache zilizopita. Ahmed ni mtu sahihi kwa Simba Sc lakini hawezi kufikia uwezo wa Manara katika suala la ushawishi kwa mashabiki wa klabu hiyo kama ilivyokua kwa Manara wakati alipokua anafanya kazi Simba Sc.

Milton Nienov Afuata Nyayo Za Manara Na Senzo Mbatha

Klabu ya Yanga bado wameendelea na utaratibu wa kuchukua watu muhimu kutoka Simba Sc ambapo siku chache zilizopita wamefanya utambulisho wa aliyekua kocha wa magolikipa wa klabu ya Simba Sc maarufu kwa majina ya Milton Nienov.

Milton Nienov anaenda kuongeza nguvu kwenye benchi la ufundi la klabu ya Yanga na hii inaonyesha wazi kwamba Yanga wamedhamiria kushinda taji la ligi msimu huu. Eng. Hersi ambaye ni mkurugenzi wa kampuni ya GSM anaendelea kutegeneza mazingira mazuri kwa Yanga kuweza kushinda taji la ligi msimu huu ili kuondoa ubabe wa Simba Sc ambao wameshinda taji la ligi kwa misimu minne mfululizo.