Home news ILI KUEPUKA KAMA YA MORRISON…YANGA WASHTUKIA JANJA JANYA YA SIMBA KWA BANGALA…WAWAHI...

ILI KUEPUKA KAMA YA MORRISON…YANGA WASHTUKIA JANJA JANYA YA SIMBA KWA BANGALA…WAWAHI AISEE…

 


YANGA ni kama wameshtukia kitu vile, ni baada ya mabosi wa timu hiyo kumuongezea mkataba wa mwaka mmoja kiraka wake Mkongomani, Yannick Bangala na kufikisha miaka miwili ya kuendelea kukipiga hapo.

Hiyo ikiwa ni siku chache tangu tetesi zienee za kiungo mkabaji wa timu hiyo, Mkongomani Mukoko Tonombe kugomea kuuzwa TP Mazembe ya nchini DR Congo.

Bangala alijiunga na Yanga katika msimu huu akitokea FAR Rabat ya nchini Morocco baada ya kuvunja mkataba wa kuendelea kukipiga huko kabla ya kutua Jangwani.

Mmoja wa mabosi wa timu hiyo, ameliambia Gazeti la Championi kuwa, kiungo huyo wiki mbili zilizopita mabosi wa timu hiyo walimuongezea mkataba wa mwaka mmoja na kufikisha miwili baada ya ule wa awali kubakisha miezi sita.

Bosi huyo alisema kuwa viongozi wa timu hiyo walishtukia kiraka huyo kuwepo katika mazungumzo na klabu yake ya zamani ya FAR Rabat aliyokuwa anaichezea.

Aliongeza kuwa pia uongozi wa timu hiyo ulishtukia kuzidiwa ujanja na watani wao Simba na haraka kumuongezea mkataba wa kuendelea kubakia kukipiga hapo kwa misimu miwili.

“Yanga ipo katika mazungumzo na baadhi ya wachezaji wake ambao mikataba yao imebakisha miezi sita na kati ya hao yupo Bangala ambaye tayari wamemuongezea mkataba wa mwaka mmoja.

“Bangala alisaini mkataba wa mwaka mmoja baadaya viongozi kuhofia kiwango chake, lakini baada ya kujiridhisha haraka wakamuongezea mkataba mwingine wa mwaka mmoja na kufikisha miwili.

“Kikubwa viongozi walihofia kutokea kile kilichotokea kama cha Morrison (Bernard) ambaye walimpa mkataba wa miezi sita wakati inaelekea kumalizika haraka Simba wakamuwahi na kumsajili,” alisema bosi huyo.

Alipotafutwa Ofisa Habari wa timu hiyo, Hassani Bumbuli kuzungumzia hilo simu yake ya mkononi iliita bila ya mafanikio ya kupokelewa.

SOMA NA HII  AL AHLY WASHIKILIA HESHIMA YA YANGA.... UONGOZI WAFUNGUKA HAYA