Home Habari za michezo HII YANGA HADI INAKERAAAH…’YAIGWAGWADUA KMC KAVUKAVU BILA CHUMVI’…ISHU NZIMA ILIKUWA HIVI…

HII YANGA HADI INAKERAAAH…’YAIGWAGWADUA KMC KAVUKAVU BILA CHUMVI’…ISHU NZIMA ILIKUWA HIVI…


KLABU ya Yanga imezidi kujikika kileleni mwa Ligi Kuu ya NBC baada ya kuifunga KMC mabao 2-0, mchezo uliochezwa kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa.

Bao la kujifunga la Andrew Vicent Chikupe na lile la Djuma Shaban yametosha kuipa Yanga pointi tatu katika mchezo huo.

Ushindi huo unawafanya Yanga wafikishe pointi 48 katika mechi 18 huku Simba wakishika nafasi ya pili wakiwa na pointi 37 kwenye mechi 17.

Safu ya ulinzi Yanga imeonekana kuwa imara licha ya mara kwa mara kubadilika wakicheza Yanick Bangala, Bakari Mwamnyeto, Dickson Job hawajaruhusu mabao kwenye mechi nane mfululizo.

Upande mwingine Yanga wanaendeleza ubabe kwa KMC baada ya mzunguko wa kwanza kuwafunga 2-0.

Yanga walianza kupata bao dakika 39 baada ya Andrew Vicent kujifunga kutokana na purukushani ya langoni kwao na mpira kumgusa mguuni na kwenda wavuni.

Kipindi cha pili KMC walifanya mabadiliko ya kuingia Abas Kapombe akichukua nafasi ya Andrew Vicent ambaye alishindwa kuendelea na mchezo baada ya kupata maumivu kwenye kipindi cha kwanza na kutolewa nje na machela.

Dakika 47 KMC walitaka kusawazisha baada ya Kipagwile kuingia ndani ya boksi na kupiga pasi ya chini chini lakini Matheo Anthony alishindwa kuuwahi na kuumalizia.

Yanga ilipata bao dakika 53 baada ya Chico Ushindi kupiga kona ya moja kwa moja na beki Djuma Shaban alionganisha kwa kichwa na mpira kwenda wavuni.

KMC walifanya mabadiliko dakika 62 wakiwatoa Kenny Ally na Matheo Anthony na nafasi zao zikichukuliwa na Charles Ilamfya na Awesu Awesu.

Wakati huo huo Kenny alionyeshewa kadi ya njano baada ya kufanya madhambi kisha akatoka nje.

Dakika 67 beki wa KMC, Hassan Kessy alionyeshewa kadi ya njano baada ya kumfanyia madhambi winga wa Yanga, Denis Nkane.

Yanga nao walifanya mabadiliko dakika 71 akitoka Denis Nkane na kuingia Deus Kaseke na dakika 73 KMC walifanya mabadiliko ya kumtoa Idd Kipagwile na kuingia Miraj Athuman.

Mabadiliko yote yalionekana kuwa wanaenda kuongeza kasi katika eneo la ushambuliaji kwa kila timu.

SOMA NA HII  GAMONDI AWAAMSHIA MABEKI YANGA KISA HIKI HAPA

Dakika 76 KMC walitaka kupata bao baada ya kugongeana na  Awesu alioiga shuti kali lakini kipa Djigui aliucheza na mpira kuwa kona isiyokuwa na faida.

Dakika 78 Yanga ilifanya mabadiliko mengine ya kumtoa Chico Ushindi na kuingia Yassin Mustapha, mabadiliko hayo yalimfanya Farid kusogea kucheza kama winga kisha Yassin alicheza beki wa kushoto.

Dakika 83 kiungo wa KMC, Masoud alionyeshewa kadi ya njano baada ya kumfanyia madhambi Fiston Mayele wa Yanga.

Dakika 86 KMC walifanya mabadiliko ya kumtoa Hassan Kabunda na kuingia Abduly Hillary lakini mchezoji huyo alionyeshewa kadi ya njano dakika 87 baada ya kumfanyia madhambi Fiston Mayele.