Home Habari za michezo KUELEKEA MECHI DHIDI YA SIMBA…MAYELE AFUNGUKA ATAKAVYOWATETEMESHA KINA ONYANGO….

KUELEKEA MECHI DHIDI YA SIMBA…MAYELE AFUNGUKA ATAKAVYOWATETEMESHA KINA ONYANGO….


MSHAMBULIAJI wa Yanga, Mkongomani, Fiston Mayele, amesema katika mchezo ujao dhidi ya Simba, wataingia uwanjani wakiwa hawana presha ya ubingwa ambayo itawafanya wacheze soka safi na kujiamini litakalowapa matokeo ya ushindi.

Mayele anayeongoza katika chati ya ufungaji Ligi Kuu Bara akifunga mabao 11, msimu huu ukiwa wa kwanza kwake kucheza hapa nchini, tayari amekutana na Simba mara mbili, akiwafunga mara moja katika Ngao ya Jamii Yanga ikishinda 1-0, huku mchezo wa ligi akishindwa kufunga matokeo yakiwa 0-0.

Mayele alisema mchezo wa raundi ya kwanza walicheza wakiwa na presha ya ubingwa ambayo ilisababisha wapate suluhu.

Mayele aliongeza kuwa, mchezo wa raundi ya pili watacheza wakiwa na presha ndogo kutokana na idadi ya pointi ambazo wanazo katika msimamo wa ligi kulinganisha na Simba.

Alibainisha kwamba, ana matumaini makubwa ya kufunga katika mchezo huo baada ya kurejea kwa wachezaji wao muhimu waliokuwa nje kwa muda ambao ni Khalid Aucho, Yannick Bangala, Feisal Salum ‘Fei Toto’ na Jesus Moloko.

“Tulianza ligi pamoja, sasa hivi sisi tupo juu na wao (Simba SC) wapo chini, tutaendelea kuwa juu na wao watabaki vilevile.

“Kikubwa sisi wachezaji tunataka ubingwa wa ligi na tulikubaliana kabla ya kukutana na wapinzani wetu katika mzunguko wa pili tuwe na tofauti ya pointi zaidi ya saba, katika hilo tumefanikiwa kwa kiasi kikubwa.

“Mechi ya kwanza ya ligi dhidi ya Simba nilicheza sikubahatika kuwafunga, lakini niliwafunga katika Ngao ya Jamii, hivyo katika mchezo wa pili wa ligi nitahakikisha ninapambana na kufunga,” alisema Mayele.

Hivi sasa katika msimamo wa Ligi Kuu Bara, Yanga imeiacha Simba pointi kumi. Yanga inaongoza ikiwa na 51, Simba inazo 41 katika nafasi ya pili.

Zimebaki mechi 11 za Ligi Kuu Bara kwa kila timu kucheza kabla ya kumaliza msimu huu.

SOMA NA HII  MABEKI HAWA WAWILI SIMBA WAZAWA NI WAZEE WA KAZI,DAKIKA KIBAO