Home Habari za michezo GWARIDE LA UBINGWA YANGA LAWA GUMZO AFRIKA…MITANDAO MIKUBWA YALIPA UZITO…WAARABU WAPAGAWA…

GWARIDE LA UBINGWA YANGA LAWA GUMZO AFRIKA…MITANDAO MIKUBWA YALIPA UZITO…WAARABU WAPAGAWA…


UMATI wa mashabiki uliojitokeza juzi Jijini Dar es Salaam kuwapokea Yanga umeishtua Afrika. Mitandao na wadau wakubwa wa soka la Afrika wameshtushwa na utitiri wa mashabiki huku Kocha Nabi Mohammed akisisitiza wanakuja na kishindo kipya kimataifa.

Yanga ambao walikabidhiwa kombe jijini Mbeya wamegeuka mjadala mkubwa kwenye michezo Afrika ambapo Istagram, Twitter wengi wameshangazwa na mapokezi makubwa ya Yanga na kudai hata klabu kubwa za Arabuni hazijawahi kufanya.

Mbali na kurasa mbalimbali za michezo Afrika, Caf wenyewe pamoja na aliyekuwa kocha wa Al Ahly, Pitso Mosimane nao wameposti na kupongeza kwa kilichotokea.

Mosimane kupitia ukurasa wake wa Twitter alisema: “Hongera Yanga, Afrika kumbe inaweza kufanya mapokezi ya taji kama zinavyofanya timu za Ulaya, tunahitaji kuona matukio mengi ya aina hii kwasababu inaonyesha mapenzi na hamasa kwa mashabiki.”

Pia mtandao maarufu wa Goal. Afrika waliweka picha ya gari iliyokuwa imebeba mataji ya Yanga na wachezaji wake na kuandika: “Ni tukio la furaha kwa Yanga mashabiki wakiwa kwenye mitaa mbalimbali ya Dar es Salaam kuipa heshima timu yao baada ya kutwaa taji la Ligi.”


Burundi, Rwanda na Morocco nako mitandao ilikuwa na picha za Yanga huku wengi wakitamani kujua kikosi chao kilivyo jambo ambalo linaashiria huenda ikaibua mchecheto kwa vigogo wengi wa Afrika ambao wameizoea zaidi Simba kimataifa. Nabi alisema usajili na maandalizi wanayotarajia kufanya yanalenga kuacha alama Afrika.

Yanga ndio mabingwa wa Tanzania na Jumamosi watacheza fainali ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Coastal Union baada ya Jumatano kumaliza ligi na Mtibwa Sugar, Uwanja wa Mkapa.

Nabi alisema; “Yanga imetwaa taji mara 28, sapoti niliyopewa kuanzia kwa wachezaji, mashabiki na viongozi naomba iendelee hasa kipindi hiki cha usajili kwa kukamilisha mapendekezo niliyoyatoa ili kutafuta rekodi nyingine kimataifa. Tunataka kufanya vizuri zaidi kimataifa msimu ujao.”

MASTAA YANGA

Nahodha, Bakari Mwamnyeto alisema; “Walichokifanya wanayanga sio cha kawaida ni historia kwenye maisha yangu, nawaahidi kuwa tutalipa deni lao kwa kufanya vizuri kwenye fainali ya Arusha.”

SOMA NA HII  SHINDA MPAKA MARA 1000 YA DAU LAKO KUPITIA SLOT YA KIJANJA YA GOD OF COINS ...

“Nimefurahi kuiongoza timu yenye malengo makubwa tulianza vizuri msimu na kuumaliza kwa furaha kwetu kama wachezaji na benchi la ufundi bila kujua kama tumebeba furaha za watanzania wengi kiasi hiki tulichoonyeshwa.”

Kiungo Feisal Salum ‘Fei toto’ alisema; “Haikuwa rahisi kwetu tunamshukuru Mungu tumekamilisha salama japo safari bado ni ndefu kwetu ila kwa ukubwa tuliopewa kutokana na mapokezi tunahitaji kulipa jasho la wananchi.”

Mjumbe wa Kamati ya Mashindano wa Yanga, Hersi Said alisema; “Tuliwaahidi ubingwa tumelifanikisha mipango iliyobaki sasa ni kufika mbali zaidi.”