Home Habari za michezo KUELEKEA MECHI ZA CAF….SIMBA , YANGA NA AZAM ZAPEWA MCHONGO HUU...

KUELEKEA MECHI ZA CAF….SIMBA , YANGA NA AZAM ZAPEWA MCHONGO HUU MWINGINE WA KWENDA MBELE…


Achana na matokeo ya jana ya Simba nchini Sudan, maandalizi ya timu hiyo na watani zao, Yanga ya Ligi ya Mabingwa Afrika yamewaibua baadhi ya makocha nchini ambao wameionya Yanga huku Simba ikipewa angalizo.

Yanga itacheza nyumbani mechi zote za awali dhidi ya Zalan ya Sudan Kusini, ambayo itaanza kuwa mwenyeji kati ya Septemba 9, 10 na 11 kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam, kabla ya marudiano.

Simba itakuwa mgeni wa Nyasa Big Bullets kwenye Uwanja wa Taifa wa Bingu, mjini Blantyre, Malawi, kati ya Septemba 9, 10 na 11 katika mchezo wake wa kwanza kabla ya kurudiana Dar es Salaam.

Maandalizi ya wawakilishi hao wa Tanzania yamewaibua baadhi ya makocha nchini, ambao wameitabiria ugumu Yanga hasa kwenye mechi za raundi ya pili, huku Simba ikipewa angalizo la kutoomba mechi yao na KMC ya Septemba 7 ya Ligi Kuu isogezwe mbele.

“KMC itawasaidia Simba kuimarisha timu, kama walikuwa na wazo la kuomba iahirishwe basi waliondoe,” alisema kocha Abdul Mingange.

Alisema Yanga itakuwa na faida zaidi kwa kuwa mechi yake ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa japo itakuwa ugenini, lakini itacheza Dar es Salaam, hivyo itakuwa na fursa ya kucheza kwanza na Azam Septemba 6 kisha kuikabili Zalan FC.

“Lakini pia ni rahisi kwa Yanga ambayo siitarajii ifungwe nyumbani mechi zote mbili, lakini itakapofuzu kucheza raundi inayofuata hapo ndipo itakutana na kigingi kwa Al Hilal (ya Sudan) au St George (ya Ethiopia), nikiyatazama maandalizi yao hivi sasa yanatia shaka tofauti na Simba,” alisema.

Alisema Yanga ina timu nzuri, lakini haipo kwenye kiwango kinachotarajiwa katika ngazi ya kimataifa, hivyo wanahitaji kujipanga ili kufika mbali zaidi tofauti na Simba, ambayo imeshiriki mfululizo na kufika robo fainali mara kadhaa.

“Hata uzoefu wa uongozi uliopo Yanga sasa kwa ngazi ya kimataifa si wa kiwango kikubwa kama ilivyo kwa Simba, ni kweli kipindi hiki wanafanya mazoezi, lakini nilitarajia wangecheza japo mechi za kirafiki kadhaa hata timu za Kenya au Zambia ambazo zingeendelea kuwaimarisha na kutengeneza muunganiko kwenye timu.

SOMA NA HII  KUHUSU ENG HERSI KUVAMIA MAJUKUMU YA CEO....UKWELI USIOSEMA HUU HAPA...SENZO ALIMKIMBIA..

“Simba ni wazoefu wa mashindano ya kimataifa kwa miaka ya karibuni, wachezaji na hata uongozi wanafahamu wapi wapite ili kufika mbali zaidi, lakini pia pamoja na kuwa wapo nje ya nchi wakicheza mechi za kirafiki, wasiache kucheza mechi yao ya Ligi ya Septemba 7, hiyo itawaongezea nguvu zaidi kabla ya mechi yao na Nyasa Big Bullet,” alisema.

Kocha Francis Baraza alisema kwa Yanga na Simba hana shaka kuwa wataanza vizuri mashindano hayo, wasiwasi wake upo kwa Azam FC, ambayo itashiriki Kombe la Shirikisho pamoja na Geita.

Baraza aliungana na Mingange kuhusu mechi ya Simba ya Septemba 7 na KMC ya Ligi Kuu akisisitiza kwamba itakuwa ni moja ya mazoezi bora kwa kocha Zoran.