Home Habari za michezo SIKU MOJA BAADA YA KUPEWA UKOCHA TAIFA STARS…MEXIME AAMUA KUFUNGUKA YA MOYONI…”HATUTAONGEZA...

SIKU MOJA BAADA YA KUPEWA UKOCHA TAIFA STARS…MEXIME AAMUA KUFUNGUKA YA MOYONI…”HATUTAONGEZA MTU”…


Siku moja baada ya kutangazwa kuwa Kocha Msaidizi wa Timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ Mecky Mexime amezungumza kwa mara ya kwanza na kueleza matarajio yake kuelekea mchezo wa Mkondo wa Pili wa kuwania kufuzu Fainali za Mataifa Bingwa ya Afrika ‘CHAN’ dhidi ya Uganda.

Taifa Stars itacheza ugenini mwishoni mwa juma hili (Septemba 03) mjini Kampala-Uganda, huku ikiwa na deni la kufungwa 1-0 katika mchezo wa Mkondo wa Kwanza uliopigwa Uwanja wa Benjamin Mkapa Jumapili (Agosti 28).

Mexime ambaye aliwahi kuitumikia Taifa Stars kama Nahodha na Beki wa kulia, amesema hana budi kulishukuru Shirikisho la Soka Tanzania kwa kumpa heshima ya kulitumikia Taifa kama Kocha.

Amesema kazi iliyo mbele yao ni kubwa, lakini watapambana ili kuisaidia Taifa Stars inayohitaji matokeo ugenini ili ifuzu Fainali za ‘CHAN’ zitakazopigwa nchini Algeria mwaka 2023.

Mexime pia amewahimiza Watanzania kuipenda Taifa Stars kwa sababu ni timu yao na hawana nyingine, hivyo ameomba ushirikiano mkubwa kutoka kwao katika kipindi hiki ambacho atakua katika Benchi la Ufundi akisaidiana na Kocha Hanour Janza ambaye ni Kocha Mkuu wa Namungo FC.

“Wacha tukapambane. Nashukuru imani ya Watanzania dhidi yangu. Lakini kubwa mashabiki waipende timu. Hatutaongeza mtu kwa muda huu ulioko, tutaenda kupambana na Uganda kwa jeshi hili hili lililoko.” amesema Mecky Mexime

Mexime kwa sasa ni Kocha Mkuu wa Kituo cha Kukuza na Kuendeleza Soka la Vijana cha Cambiasso kilichopo jijini Dar es salaam. Pia aliwahi kuzinoa timu za Kagera Sugar na Mtibwa Sugar zinazoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara.

SOMA NA HII  AFISA HABARI SIMBA AFUNGUKA ISHU YA YANGA KUMTAKA AENDE KWAO...AGUSI ISHU YA KUFUKUA MAFAILI...