Home Habari za michezo PAMOJA NA KUFANYA MAKUBWA….MGUNDA AWAPA MTIHANI MZITO MABOSI SIMBA…

PAMOJA NA KUFANYA MAKUBWA….MGUNDA AWAPA MTIHANI MZITO MABOSI SIMBA…

Habari za Simba

Kiwango kizuri anachokionyesha Kocha Mkuu wa Simba, Juma Mgunda tangu apokee mikoba ya Zoran Maki ni kama mtego kwa viongozi wa timu hiyo, kufanya maamuzi ya kusaka kocha mpya wa kigeni.

Kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika, Mgunda amesimamia mechi tatu akicheza na Nyasa Big Bullets ya Malawi, ugenini alishinda mabao 2-0, wafungaji wakiwa ni Moses Phiri na John Bocco, wakipewa asisti na Clatous Chama, Uwanja wa Mkapa, walishinda mabao 2-0 yakifungwa na Phiri asisti ya kwanza ilikuwa ya Chama na ya pili ni Augustine Okra.

Mgunda amekwenda kudhihirisha ubora wake zaidi baada ya kwenda kuichapa C.D Primeiro de Agosto ugenini mabao 3-1, mabao hayo yalifungwa na Chama, Israel Mwenda, Phiri asisti ya Chama.

Kwa upande wa mechi za Ligi Kuu Simba ilishinda dhidi ya Prisons bao 1-0 (Sokoine) na Dodoma Jiji waliichapa mabao 3-0 (Mkapa).

Kutokana na matokeo hayo, inaonyesha namna Mgunda alivyofanikiwa kutengeneza pacha kati ya Phiri na Chama, pia ameimalisha safu yake ya ulinzi ambayo imeruhusu bao moja tu, huku jumla ya mabao ya Ligi Kuu yakiwa manne na CAF 7-1.

Kutokana na mwenendo wake, beki wa zamani wa timu hiyo, Kassongo Athuman alisema kama Mgunda amefanikiwa kuirejesha Simba kwenye mstari anastahili kuaminiwa na kupewa sapoti na mashabiki pamoja na viongozi.

“Kwanza nawaona wachezaji amewarudisha kwenye morali ya kazi, unaona wanajituma tofauti na awali, hivyo mashabiki na wadau wa Simba, tunapaswa kumpa heshima yake kama mzawa ameweza kutupa furaha,” alisema.

Kauli yake iliungwa mkono na beki wa zamani wa Yanga, Willams Mtendamema aliyesema Mgunda alionekana kutoaminika, lakini ameonyesha anawajua vizuri wachezaji na ameweza kuishi nao na kuwarejesha mchezoni.

“Mgunda amefanikiwa kwa asilimi kubwa, mfano mechi ya waliyokwenda kucheza Angola nani alitarajia Simba ingepata ushindi mnono na wa kishindo, wengi wao walijua wangefungwa, ila Mgunda kaonyesha utofauti wa kuvuka hivyo vikwazo, binafsi naona anastahili kuaminiwa na viongozi wa Simba,” alisema.

SOMA NA HII  KIBOKO YA MANULA NA AYOUB ATAKIWA MSIMBAZI....JAMAA NI BALAA NA NUSU...