Home Habari za michezo TUNZA HII…MUDATHIR YAHYA KUMFUATA NTIBAZONKIZA SIMBA SC…ISHU NZIMA IKO HIVI…

TUNZA HII…MUDATHIR YAHYA KUMFUATA NTIBAZONKIZA SIMBA SC…ISHU NZIMA IKO HIVI…

Mudathiri yahya kujiunga Simba SC

Simba SC imeendelea kushusha majembe usajili wa dirisha dogo, baada ya kumtangaza mpika mabao Said Ntibanzonkiza wakimpa kandarasi ya mwaka mmoja na nusu, na kuanzia sasa atatangazwa fundi mwingine ndani ya klabu hiyo.

Imeelezwa tayari wamemalizana na kiungo Mudathir Yahya anayemudu kucheza nafasi mbili – namba sita na nane uwanjani, akiwa mchezaji huru baada ya kuachana na Azam FC kabla msimu haujaanza.

Mudathir ambaye alikuwa akifanya mazoezi na KMKM ya Zanzibar, alianza kuhusishwa na timu yake ya zamani Azam FC, Yanga na sasa Simba SC kuifanikisha saini yake, watalamu wa soka wameona kuna jambo anakwenda kuliongeza ndani ya kikosi hicho.

Chanzo cha kuaminika kutoka ndani ya klabu hiyo kimethibitisha kuwa staa huyo muda wowote atatangazwa ndani ya timu hiyo, ambayo ina mastaa sita eneo la kiungo mkabaji.

“Ni kiungo mzuri atakuja kuongeza kitu ndani ya timu uwepo wa Sadio Kanoute, Jonas Mkude na Mzamiru Yassin, hauwezi kuondoa kuongezwa wachezaji wengine kwani Simba SC ni timu kubwa ina mashindano mengi pia kuna kuumia kwa mchezaji, hivyo lazima mbadala awepo ambaye pia ana kiwango kikubwa,” kilisema chanzo hicho.

“Hili ni dirisha la usajili ambalo lipo kwa ajili ya kuboresha kikosi kutokana na kile kilichofanyika kwenye michezo ya mwanzoni mwa msimu, kocha kapendekeza ongezeko la mchezaji eneo hilo hatujakurupuka.

“Kuhusu idadi kubwa muda bado upo kutakuwa na kupunguza baadhi ya wachezaji ambao watatolewa kwa mkopo kutokana na kushindwa kuonyesha kile tulichokuwa tunatarajia kutoka kwao.”

Chanzo hicho kilisema, Simba SC ina mpango wa kuwatoa wachezaji wawili kwenye eneo hilo kwa mkopo ambao ni pamoja na Nassoro Kapama na Victor Akpan, kutokana na kukosa nafasi kabisa ya kuonyesha uwezo wao tangu waliposajiliwa ndani ya timu hiyo.

Ongezeko la Mudathir ndani ya timu hiyo linaongeza ushindani wa namba kwa wawakilishi hao wa mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika ili kupata kikosi bora zaidi.

MAKOCHA WATIA NENO

Mchezaji na kocha wa zamani wa Simba SC, Abdallah Kibaden alisema ongezeko la mchezaji ndani ya timu hiyo ni mipango ya kocha, hawezi kuzungumzia kiufundi lakini anaamini ujio wake utaongeza kitu huku akisisitiza kuwa ana imani na wazawa.

“Kuna wachezaji wanachukuliwa kutoka nje wanakuja kuharibu nafasi za wazawa,” alisema Kibadeni.

Kocha wa zamani wa Biashara na Kagera Sugar, Francis Baraza alisema kila mchezaji ana umuhimu wake kwa wakati husika kutokana na kuwa na utofauti. Simba SC iliingia jana jijini Dar ikitokea Mwanza ambako iliibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya KMC.

SOMA NA HII  KOCHA MTIBWA SUGAR AOMBA WIKI MBILI