Home Habari za michezo SIMBA NA YANGA ZAZIDI KUINGARISHA TZ CAF……ISHU IKO HIVI…

SIMBA NA YANGA ZAZIDI KUINGARISHA TZ CAF……ISHU IKO HIVI…

Habari za Simba na Yanga

Michuano ya Ligi ya Mabingwa na Kombe la Shirikisho Afrika, imefikia patamu wakati mechi za makundi zikiwa raundi ya nne, huku Raja Casablanca na US Monastir zikiwa zimejihakikisha kutinga robo fainali, lakini wawakilishi wa Tanzania, Simba na Yanga zikifunika katika michuano hiyo.

Timu hizo zimekuwa ni tishio kwa vigogo wakubwa baada ya kupiga pasi nyingi katika michezo yao ya michuano huyo Yanga ikiwa Kundi D ya Kombe la Shirikisho na Simba iliyopo Kundi C inashiriki Ligi ya Mabingwa Afrika zote zikitangulia mguu mmoja kwenye robo fainali hadi sasa.

Rekodi zinaonyesha timu hizo kwenye mechi nne za makundi zuimefanya vizuri kwenye klupiga pasi nyingi licha ya kila moja kuanza vibaya mechi zao za kwanza kwa kupoteza zikicheza ugenini.

Mwanaspoti linakuletea namna timu hizo zilivyofanya vizuri kwenye upigaji wa pasi na kuvifunika vigogo.

SIMBA Licha ya mashabiki wa Simba kupiga kelele kwa kutoridhishwa na mwenendo wa timu hiyo, ila hadi sasa hii ndio timu inayoongoza kwa kupiga pasi nyingi zaidi katika Ligi ya Mabingwa (hii ni kabla ya mechi za jana za ligi hiyo).

Simba yenye pointi sita nyuma ya Raja Casablanca ya Morocco yenye 12 imepiga jumla ya pasi 1901 katika michezo minne iliyocheza ikihitaji pointi tatu kutinga robo fainali.

Mchezo wake wa kwanza dhidi ya Horoya uliopigwa Februari 11, kwenye Uwanja wa General Lansana Conte Guinea, licha ya kupoteza bao 1-0 ila ilipiga pasi 413 wakati wapinzani wao walipiga 338.

Katika mchezo wake wa pili uliopigwa Februari 18 dhidi ya Raja Casablanca kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Simba ilichapwa mabao 3-0 ingawa ilipiga pasi nyingi 523 huku Raja ikipiga 324.

Ushindi wa kwanza kwa Simba katika hatua hii ulikuwa ni wa bao 1-0 dhidi ya Vipers Februari 25 kwenye Uwanja wa St. Mary’s nchini Uganda ikipiga pasi 396 wakati wapinzani wao walipiga 368.

Simba iliendeleza wimbi la ushindi na kufufua matumaini ya kusonga mbele baada ya mchezo wake wa nne kushinda pia 1-0 na Vipers Machi 7, Uwanja wa Benjamin Mkapa ikipiga pasi 569 kwa 324.

Mbali na Simba timu inayoshika nafasi ya pili ni Esperance ya Tunisia iliyoko kundi ‘D’ kwenye michuano hii ambayo katika michezo yake minne iliyocheza hadi sasa imepiga jumla ya pasi 1874.

Ya tatu ni Raja Casablanca iliyokuwa kundi moja na Simba iliyopiga jumla ya pasi 1753 ikiwa ni ya kwanza kufuzu robo fainali baada ya kushinda michezo yake yote minne na kufikisha pointi 12.

Mabingwa wa kihistoria mara 10 Al Ahly kutoka Misri iliyopo kundi A baada ya kucheza michezo mitatu (kabla ya jana )i mepiga pasi 1585 wakati Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini imepiga 1678.

YANGA Katika Kombe la Shirikisho Yanga inashika nafasi ya tatu kwa kupiga pasi nyingi ikiwa na jumla ya pasi 1741 nyuma ya vinara Pyramids ya Misri na FAR Rabat (Morocco) zilizopiga pasi 2102 kutoka Kundi C.

Yanga ilianza vibaya mchezo wa kwanza ugenini kwa kupoteza mabao 2-0 na Monastir ya Tunisia kwenye Uwanja wa Olympique De Rades Februari 12.

Licha ya kufungwa mchezo huo ila Yanga ilipiga jumla ya pasi 539 ikiwa ni nyingi zaidi kuliko za wapinzani wao ambao licha tu ya kushinda ikiwa dimba lake la nyumbani ila ilipiga pasi 376.

Mchezo wa pili uliopigwa kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa Februari 19, Yanga ilishinda kwa mabao 3-1 dhidi ya TP Mazembe kutoka DR Congo ikipiga jumla ya pasi 367 huku wapinzani wakipiga 346.

Februari 26 ikicheza nchini Mali dhidi ya AS Real Bamako ililazimishwa sare ya bao 1-1 ingawa ilitawala pia mchezo baada ya kupiga jumla ya pasi 442 kwa 352 zilizopigwa na wapinzani wao.

Kwenye ushindi wa mabao 2-0 ilioupata dhidi ya Real Bamako kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa Machi 8 na kuweka matumaini yake hai ya kufuzu robo fainali ilipiga jumla ya pasi 393 kwa 350.

Timu nyingine zilizopiga pasi nyingi ni Future (Misri) iliyopiga 1701 na ASKO Kara ya nchini Togo ambayo nayo imepiga 1694 ambapo zote zinatokea kundi la ‘C’ lenye Pyramids na FAR Rabat.

SOMA NA HII  PAMOJA NA KUTOPEWA UKOCHA MKUU MPAKA SASA...MGUNDA KAAMUA KUFUNGUKA SIRI ZAKE NA SIMBA...