KIUNGO wa Ihefu, Papy Kabamba Tshishimbi huenda asirejee tena uwanjani katika michezo yote iliyosalia msimu huu baada ya kutakiwa kupumzika kufuatia kufanyiwa upasuaji mkubwa wa goti.
Akizungumza na SOKA LA BONGO, kocha msaidizi wa Ihefu, Zubery Katwila alisema ni bahati mbaya kwa kiungo huyo wa zamani wa Yanga kutoka Dr Congo kama mchezaji na wao kama benchi la ufundi kwani bado walikuwa wanahitaji huduma yake.
“Kwa yeye kurudi msimu huu ni ngumu ndio maana tukaona ni vyema tumpe muda mwingi wa kupumzika ili arudi akiwa imara zaidi, hivyo tunararajia kuanzia sasa ataanza mazoezi mepesi mepesi tu.”
Kwa upande wa Katibu Mkuu wa Klabu hiyo, Zagalo Chalamila alisema baada ya Tshishimbi kufanyiwa upasuaji jijini Dar es Salaam aliomba kwenda kwao, hivyo kuanzia wiki hii atarudi nchini.
“Mwezi uliopita alituomba aende kwao kwa ajili ya kuangaliwa zaidi na kupatiwa matibabu nasi kama viongozi tulimpatia hiyo ruhusa hivyo tunamtarajia kurudi muda wowote kuungana na wenzake.”