BEKI Pascal Wawa wa Singida Big Stars ameweka wazi kuwa mmoja wa washambuliaji ambao anawaona wana kitu kikubwa kwenye Ligi Kuu Bara ni Fiston Mayele anayecheza katika kikosi cha Yanga.
Wawa amesema Mayele ni mshambuliaji ambaye kama beki unapokutana naye inabidi utumie akili kubwa kukabiliana naye kwa sababu amekamilika anapokuwa ndani ya uwanja akiitetea timu yake.
“Mayele ni mchezaji mwenye nguvu, spidi na analijua sana goli kwa hiyo kwenye kukabiliana naye lazima uwe na kitu cha ziada, ni mchezaji mzuri sana kwa washambuliaji ambao wapo kwenye ligi hapa;
“Namuombea kwa Mungu aendelee kufanya vizuri atoke pale alipo na aende sehemu ambayo ataendelea kupata pesa nyingi ili familia yake izidi kujivunia kuhusu yeye.”
Wawa alisema alishawahi kukutana na mchezaji huyo nje ya uwanja alipokwenda kumtembelea mchezaji mwenzake wa Singida Bs (Francis Kazadi) ambaye ni raia wa DR Congo.
“Nilikutana naye nje ya uwanja nilikuwa nyumbani kwa Kazadi wakati huo tulikuwa na mapumziko mafupi Dar, alinikuta pale alikuja kulikuwa na wezake wengine ni mchezaji ambaye ana utu sana;
“Mchangamfu na tulipiga stori kama vile tunafahamiana kwa hiyo hata nje ya uwanja ni mtu mzuri kwa sababu tulikuwa kama watu ambao tunafahamiana kwa muda mrefu.”