BAADA ya kukaa nje ya uwanja wa muda, kiungo mshambuliaji wa Simba, Augustine Okrah ambaye aliifunga Yanga kwenye sare ya bao 1-1 mzunguko wa kwanza ameomba kucheza mechi ya Aprili 16.
Okrah alikuwa nje ya uwanja wiki nne akiiguza kidole kwenye ambacho alivunjika kwenye mchezo wao wa kirafiki dhidi ya Al Hilal, amerudi na anatarajia kuungana na kikosi cha timu hiyo kambini tayari kwa ajili ya kujiandaa na mchezo dhidi ya Ihefu FC.
Akizungumza na soka la bongo, Okrah alisema yupo fiti na ameshaanza mazoezi binafsi akianzia gym na leo anatarajia kuungana na timu na kuendelea na mazoezi kuhusu kucheza anamuachia kocha lakini kwa upande wake yupo tayari kupambana.
“Namshukuru Mungu naendelea poa sasa baada ya kukaa nje ya uwanja kwa muda nimesharuhusiwa kuanza mazoezi na nitaungana na timu kesho ‘leo’ baada ya timu kurejea kutoka mapumziko;
“Natamani kupata nafasi ya kucheza mechi sita za ligi zilizobaki ili kujiweka katika mazingira mazuri kutokana na kukosekana na muda mrefu na kuhusiana na ratiba iliyopo kuna mechi dhidi ya Yanga Aprili 16 naitamani sana ukweli naomba kocha anipe jezi kwenye mechi hii.” alisema.