Home Habari za michezo MSHAHARA WA MORISSON KUMLIPA LILEPO YANGA…..DILI ZIMA LINASUKWA KIMYA KIMYA…

MSHAHARA WA MORISSON KUMLIPA LILEPO YANGA…..DILI ZIMA LINASUKWA KIMYA KIMYA…

Tetesi za Usajili Bongo

YANGA imeshtua kwa kumpiga chini winga, Bernard Morrison ambaye mwishoni mwa msimu huu alianza kuwaka, lakini hawakujali hilo na wakampa ‘thank you’ ili akasake klabu nyingine, wakati Mghana huyo anatoka kuna vuma viwili wataingia fasta.

Hesabu kali za Yanga baada ya kumpiga chini Morrison bosi wao mkubwa wa klabu, Injinia Hersi Said ambaye ndiye stelingi wa vita ya usajili kuna hesabu kubwa anaweza kuzipiga kufuatia kupatikana nafasi ya Morrison.

Morrison akiwa Yanga ndiye aliyekuwa analipwa fedha ndefu akichukua Dola 10,000 (Sh 23 milioni) kwa mwezi hatua ambayo mabosi wa Yanga wanaona kazi aliyoifanya kwa msimu uliopita haiendani na kiasi alichokuwa anachukua.

Yanga sasa wanataka kutumia mshahara huo wa Morrison kuipigania saini ya winga Makabi Lilepo wa Al Hilal ya Sudan ambaye walikuwa wakishindana naye mshahara.

Endapo Yanga watafanikiwa kumnasa Lilepo watakuwa wameziba nafsi ya Morrison kwa mtu wa maana ambaye atawaongezea ubora mkubwa kwenye safu yao ya ushambuliaji kwa msimu ujao.

Inafahamika kwamba Hersi yuko kwenye mawasiliano mazuri na Lilepo sio kwasasa pekee hata kabla ya kutua Sudan aliwahi kuhitaji huduma yake akiwa klabu yake ya zamani ya AS Vita.

Mbali na Lilepo, Yanga pia inataka kurudi kwa rafiki zao Union Maniema kumchukua winga mwingine wa kulia Maxi Mpia Nzengeli.

Maxi ambaye ni nahodha wa Maniema anasifika kwa kasi, pia akijua kutengeneza pasi za mabao akiwa na klabu yake, huku akiwa kwenye kikosi cha DR Congo kilichoshiriki Fainali za Mataifa Afrika kwa wachezaji wa ndani CHAN.

Maxi ni winga ambaye ataweza kuziba nafasi iliyoachwa wazi na Tuisila Kisinda anayerudishwa klabu yake ya RS Berkane ya Morocco baada ya muda wa mkataba wake wa mkopo wa mwaka mmoja kumalizika.

Yanga haitatumia nguvu kubwa kumnasa Maxi kwani tayari klabu hizo mbili ziko kwenye ushirikiano mzuri wa kuuziana wachezaji kama ambavyo walifanya kwa Mukoko Tonombe, Kisinda na Jesus Moloko ambao walitokea AS Vita lakini wakiwa ni wachezaji wa Maniema.

SOMA NA HII  KUHUSU MBRAZILI SIMBA KUMKUBALI GHAFLA....MINZIRO AANIKA 'UCHAWI' ANAOTUMIA KIBU DENIS..