Home Azam FC FT:YANGA WAPITA MULEMULE WALIKOPITA SIMBA….WABEBA NDOO NYINGINE KIBABE….

FT:YANGA WAPITA MULEMULE WALIKOPITA SIMBA….WABEBA NDOO NYINGINE KIBABE….

Yanga Bingwa FA

Yanga imebeba tena. Kenedy Musonda ndiye aliyeipatia bao la ubingwa wa Kombe la Shirikisho la Azam akifunga bao hilo dakika ya 16 ya mchezo.

Mchezo huo wa fainali ulifanyika uwanja wa Mkwakwani jijini hapa ambapo Musonda alifunga bao hilo kwa kichwa baada ya kuunganisha krosi ya Tuisila Kisinda.

Musonda alikosa bao dakika ya 20 kwani alipiga shuti akiwa nje ya 18 na kutoka nje akiwa amepokea pasi ya Bernard Morrison wakati huo mchezaji wa Azam, Ayoub Lyanga naye akikosa bao dakika ya 27 akipiga mpira wa faulo uliodakwa na kipa Djigui Diarra.

Faulo hiyo kwa Azam ilitokana na Khalid Aucho kumfanyia madhambi James Akaminko huku Yanga nao wakipata mpira wa faulo uliopigwa na Morrison baada ya Tuisila kuchezewa faulo ikiwa ni dakika ya 34.

Mwamuzi wa mchezo huo Ramadhan Kayoko alimpa kadi ya njano mchezaji wa Yanga, Dickson Job kwa kumchezea rafu Iddris Mbombo wa Azam.

Kipindi cha pili kocha wa Azam FC, Naskali Ongalo alifanya mabadiliko akiwatoa wachezaji wawili kwa wakati mmoja, Ayoub Lyanga nafasi yake ilichukuliwa na Kipre Junior, Bruce Kangwa aliingia Pascal Msindo.

Naye kocha wa Yanga, Nasredinne Nabi akifanya mabadiliko ya kumtoa Tuisila nafasi yake ilichukuliwa na Mudathir Yahya

Morrison aliyeonekana kama amechoka alikosa bao dakika ya 59 kwani shuti lake alipiga nje kidogo ya goli huku Azam nao kupitia mshambuliaji wao Abdul Seleman ‘Sopu’ akipiga shuti lilipita juu kidogo ya goli akiwa na kipa ikiwa ni dakika ya 70 na 71 Azam walifanya shambulizi lingine lakini halikuwa na madhara kwa Yanga.

Nabi aliendelea kufanya mabadiliko kwa lengo la kupata mabao zaidi ambapo aliwatoa Morrison nafasi yake ilichukuliwa na Clement Mzize huku Yanick Bangala akiingia kuchukuwa nafasi ya Salum Abubakar ‘Sure Boy’, Mzize alifanya jaribio la kwanza la kufunga bao mara tu ya kuingia dakika ya 78 lakini shuti lake lilipita juu ya mwamba.

Dakika ya 87, Kayoko alitoa kadi ya njano kwa Musonda aliyemfanyia madhambi Akaminko huku Kibwana Shomari akiingia kuchukuwa nafasi ya Shaban Djuma huku Azam akiingia Idd Seleman akitolewa Sospeter Bajana ikiwa ni dakika ya 89.

Kwenye michuano hii ya ASFC, Yanga na Azam hazijakutana mara nyingi, zimekutana mara moja msimu wa 2015/16 Yanga ilishinda mabao 3-1 huku Azam yenyewe ikichukuwa ubingwa wa mashindano hayo mara moja msimu wa 2018/ ilipoifunga Lipuli bao 1-0.

Yanga ilikuwa inatetea ubingwa wao kwani msimu uliopita ilishinda kwa penalti 4-1 dhidi ya Coastal Union baada ya dakika 90 kufungana mabao 3-3.

Tangu michuano hiyo ilipobadilishwa jina nakuitwa ASFC mwaka 2015, Simba ndio timu pekee inayoongoza kulichukua taji hilo imechukua mara tatu kuanzia msimu wa 2016/17, 2019, 2020 na 2020/21 wakati Yaga ikichukuwa mara mbili msimu wa 2015/16 na 2021/22.

Kiujumla tangu michuano hiyo iliopoanza ikiitwa FAT mwaka 1967 na sasa ASFC, Yanga ndio timu pekee inayoongoza kulichukua mara nyingi taji hilo kwani imechukua mara sita (6) kuanzia 1967, 1974, 1998, 2001, 2015/16 na 2021/22.,

Simba inafuatia ikichukua mara nne (4) kuanzia 1995, 2016/17, 2019/20 na 2020/21.

VIKOSI

Azam

Iddris Abdilai, Lusajo Mwaikenda, Bruce Kangwa, Abdallah Kheri, Daniel Amour, Issah Aliyu, Abdul Suleiman, Sospeter Bajana, Iddris Mbombo, James Akaminko na Ayoub Lyanga

YANGA

Djigui Diarra, Shaban Djuma, Joyce Lomalisa, Ibrahim Abdallah, Bakari Mwamnyeto, Dickson Job, Tuisila Kisinda, Khalid Aucho, Kennedy Musonda, Salum Abubakar, Bernard Morrison

SOMA NA HII  KUELEKEA MECHI ZA CAF...EDO KUMWEMBE AWAPASULIA UKWELI HUU YANGA...