Home Habari za michezo ENG, HERSI SAID AFUNGUKA SABABU HIZI ZA KIBABANGE KUTUA YANGA

ENG, HERSI SAID AFUNGUKA SABABU HIZI ZA KIBABANGE KUTUA YANGA

Tetesi za Usajili Yanga

Rais wa Klabu ya Yanga, Eng. Hersi Said amesema kuwa sababu kubwa ya kumsajili beki Nickson Kibabage ni kutengeneza wigo wa kuwa na wachezaji wengi wazawa ili kuwapa nafasi ya kuzitumikia timu kubwa na baadaye Timu ya Taifa.

Hersi amesema hayo ikiwa ni saa chache baada ya Kibabage kutangazwa kusajiliwa Yanga akitokea Singida Fountain Gate na tayari ameshaondoka na kikosi cha timu hiyo kwa ajili ya kwenda Malawi kwenye mchezo wa kirafiki na Nyasa Big Bullets wakati wa sherehe za maadhimisho ya Uhuru wa Taifa hilo.

“Wapo wachezaji kadhaa tumewasajili kwa ajili ya kuboresha kikosi chetu kuelekea msimu ujao na Kibabage ni miongoni mwa wachezaji hao. Sisi tumekuwa tukiangalia mahitaji gani ambayo tunayo kwenye timu na ku-promote wachezaji wetu wa ndani kucheza kwenye hizi timu kubwa.

“Itakumbukwa kuwa msimu uliopita hatukuwa na mchezaji yoyote tuliyemsajili kwenye dirisha kubwa, ni mapenzi yetu kama viongozi kukuza vipaji vya wachezaji wetu hapa nchini.

“Ni fahari kubwa kumsaini Kibabage ambaye amepitia kwenye misingi yote ya malezi ya soka kuanzia Under 17 mpaka Under 20, ni mchezaji ambaye ameandaliwa vizuri katika malezi yake ya soka.

“Juzi tulimsikia Rais Mstaafu Mzee Jakaya Kikwete akisema ni wakati sasa wa kuwakuza wachezaji wetu wa ndani, kwa hiyo ni fahari kwetu kumsaini Kibababge, kijana wa Kitanzania kuja kupata platform ya kucheza Yanga, klabu kubwa nchini inayoshiriki michuano ya Kimataifa na kupigania Ubingwa wake.

“Kibabage atapata uzoefu mpya, majukumu mapya na malengo mapya tofauti na alikokuwa ambako pengine hakukuwa na malengo ya ubingwa, hapa kila mechi atakayocheza malengo makuu ni kushinda, atacheza na wachezaji wazuri na hata kukuza ubora wake,” amesema Hersi.

SOMA NA HII  SIMBA HATA WAONGEZA POINTI KIASI GANI, YANGA ITAWASHUSHA TU. KAMWE