Home Habari za michezo SIRI YA DUCHU KUREJEA SIMBA YATAJWA, MWENDA KAPOMBE WAHUSISHWA

SIRI YA DUCHU KUREJEA SIMBA YATAJWA, MWENDA KAPOMBE WAHUSISHWA

SIMBA iko nchini uturuki ilikokita kambi maalumu ya kujifua kwaajili ya msimu ujao iliopanga kufanya mapinduzi na kurejesha ufalme wake uliotwaliwa na watani zao wa jadi Yanga kwa misimu miwili iliyopita.

Wakati ikiendelea kujifua kule uturuki, ndani ya kikosi cha Simba kuna sura mpya za makocha na wachezaji lakini pia yupo kijana David Kameta ‘Duchu’ aliyerudi msimbazi baada ya kukaa nje ya kikosi hicho kwa misimu miwili.

Duchu alisajiliwa na Simba kwa mara ya kwanza msimu wa 2020/2021 akitokea Lipuli, lakini alidumu kikosini hapo kwa msimu mmoja kabla ya kupelekwa kwa mkopo Biashara United kisha Geita Gold na baadae Mtibwa Sugar.

Baada ya misimu miwili mbali na jezi ya Simba, sasa amerejea kwa wakali hao wa Msimbazi tena na amepewa kandarasi ya miaka mitatu huku wenye Simba yao wakiamini ameiva sasa tayari kwa kuwatumikia kwa asilimia 100.
Kupitia Makala haya, hizi ni sababu tano ambazo zimemfanya Duchu kurejea Simba kwaajili ya msimu ujao na endelevu.

MAHITAJI
Simba katika nafasi anayocheza Duchu (Beki wa kulia) kuna mabeki wawili asilia, Shomari Kapombe na Israel Mwenda lakini pia Jimmyson Mwanuke mara kadhaa amekuwa akicheza eneo hilo kama kiraka.
Hata hivyo, Kapombe ndiye anaonekana kujitengenezeaq utawala katika eneo hilo kulingana na Mwanuke na Mwenda kushindwa kuonyesha ushindani mkubwa kwake.
Hivyo Simba ilihitaji beki atakayetoa ushindani kwa Kapombe ambapo kwa wazawa, Duchu ni miongoni mwa wachezaji waliokuwa bora katika misimu miwili iliyopita na wanaweza kutoa ushindani kwa Kapombe na hata kuwa mbadala bora katika eneo hilo.

UBORA
Jambo lingine lililochagiza Duchu kurejea Simba ni ubora aliounyesha tangu ametolewa kwa mkopo hadi msimu uliopita akiwa Mtibwa.
Kumekuwa na uchache wa mabeki wa kulia nchini wenye muendelezo wa ubora wao kwenye ligi hususani vijana.
Wengi wamekuwa wachezaji wa msimu mmoja na misimu mingine wanazingua lakini Duchu ubora wake umekuwa na muendelezo na kila uchwao anaonekana kuimarika zaidi jambo lililowashawishi Simba kumrejesha kundini na kuachana na dili nyingine.

NONGWA ZA MWENDA & KAPOMBE
Ni ngumu kwa kiongozi wa Simba, Kapombe au Mwenda kutoka nje na kusema wiwili hao hawapo kwenye mahusiano mazuri lakini ‘Watu wa boli’ wanajua na kutambua nini kinaendelea kati yao.
Ni ukweli kuwa Kapombe na Mwenda kuna mambo binafsi yaliwafanya wapishane mitazamo na kauli na kujenga uhasama ambao waswahili wanasema; “Wanachekeana usoni lakini moyoni wanachukiana”.

Hilo limetosha kwa Simba kuhitaji mtu mwingine atakayekaa katikati yao na Duchu ndiye ameingizwa hapo.
Mwanaspoti linajua Simba ilijaribu kuwapatanisha wawili hao lakini wakamaliza tofauti zao kishingo upande na sasa kinachofuata Mwenda huenda akahamia upande wa beki ya kushoto anakocheza Mohamed Hussein ‘Tshabalala’.

MAHUSIANO BORA
Mara nyingi wachezaji wanaocheza, Simba na Yanga kisha kuondoka wamekuwa wakiharibu uhusiano baina yao na taasisi hizo aidha kwa kuzisema vibaya au kunyooshea vidole baadhi ya watu.
Hali ilikuwa tofauti kwa Duchu kulingana na moja ya kiongozi wa Simba (Jina tunalo), alithibitisha kuwa moja ya sababu zilizomrudisha Simba.
“Tumekuwa tukifuatilia, mwenendo wa kila mchezaji wetu tunayemtoa kwa mkopo kuanzia ubora hadi tabia, Duchu amekuwa balozi mzuri kwetu na ndio maana lilipokuja jina lake hatukusita kumpitisha,” alisema kiongozi huyo.

NIDHAMU
Jambo lingine lililomrudisha Duchu Simba ni nidhamu yake ndani na nje ya uwanja.
Maisha ya Simba yanahitaji nidhamu ya hali ya juu ili kuyamudu na kuendana na matakwa.
Tangu Duchu anatua sima misimu mitatu iliyopita aliweza kuwa na nidhamu ya hali ya juu na kwendana vyema na matakwa ya timu, changamoto ikawa ushindani mkubwa aliokutana nao kutoka kwa Kapombe.

Hata alivyotoka Simba aliendelea kuwa na nidhamu kubwa kama mchezaji na amekuwa na kiu ya kufanya vizuri zaidi jambo ambalo limewafanya viongozi wa msimbazo kumpa miaka mitatu tena.

Akizungumza baada ya kujiunga tena na Simba Duchu aliushukuru uongozi wa timu hiyo kwa kumuamini na kumpa nafasi tena huku akiahidi kufanya vizuri zaidi.
“Nina furaha kurejea hapa, nadhani ni wakati wa kupambana zaidi ili kuifanya timu ifikie malengo yake, pia mimi kufikia malengo binafsi, mambo ninayoamini kwa kushirikiana na wachezaji wenzangu tutatayatimiza,” alisema Duchu.

SOMA NA HII  HAKIKISHA JINA LINATOKA BALEKE