Home Habari za michezo BAADA YA KUANZA KUTUPIA TENA….PHIRI KATUMA UJUMBE HUU KWA MABEKI LIGI KUU…

BAADA YA KUANZA KUTUPIA TENA….PHIRI KATUMA UJUMBE HUU KWA MABEKI LIGI KUU…

Habari za Simba

MSHAMBULIAJI wa Simba, Mzambia, Mosses Phiri, ametangaza hali ya hatari kwa mabeki wa timu za Ligi Kuu Bara zikiwemo Yanga na Azam kwa kuwaambia amejipanga kufunga mabao katika kila mchezo atakaopewa nafasi ya kucheza msimu huu ili kurudisha ubora wake uliopotea.

Phiri ametoa kauli hiyo kufuatia bao lake la ushindi alilofunga juzi Jumapili katika mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Dodoma Jiji kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar, wakati Simba ikishinda 2-0.

Phiri alisema amefurahi kufunga bao lake la kwanza kwenye mechi ya kwanza msimu huu baada ya msimu uliopita kumaliza vibaya akiuguza majeraha.

“Nafurahi kufunga bao langu la kwanza, nina imani kushirikiana na wenzangu nitawapa furaha mashabiki wa Simba na kuhakikisha tunapambana kufikia malengo wanayoyatarajia ikiwemo kushinda kila mechi.

“Matarajio yangu ni kufunga zaidi kila ninapopata nafasi ya kucheza, msimu uliopita nilifunga mabao kumi na sikuweza kuendelea kwa sababu ya majeraha, nina imani na kumuomba Mungu anijaalie afya njema ili niweze kukata kiu ya mashabiki wetu,” alisema Phiri.

Ikumbukwe kuwa, Phiri mkali wa kutupia kwa kutumia guu la kulia, amefunga bao hilo baada ya kupitisha saa 6,240 bila kuonesha makeke yake.

Ikumbukwe kuwa saa hizo 6,240 ambazo zinapatikana ndani ya siku 260, mwamba Phiri hakupata zali la kufunga kwenye mechi za ligi. Rekodi zinaonesha mara ya mwisho Phiri kufunga ni Desemba 3, 2022 Uwanja wa Mkwakwani, Tanga. Alifunga mabao mawili dakika ya 53 na 60.

Maumivu aliyopata kwenye mchezo wa ligi dhidi ya Kagera Sugar, Desemba 21, 2022 Uwanja wa Kaitaba, Kagera, yalimpunguzia kasi yake kwani licha ya kupona na kuanza kurejea uwanjani bado hakupata nafasi ya kutupia, kabla ya Agosti 20, akitokea benchi dhidi ya Dodoma Jiji, kupachika bao lake la kwanza msimu wa 2023/24 dakika ya 55.

SOMA NA HII  YANGA YATEMBEZA MKWARA,KUISIMAMISHA NCHI NA AFRIKA...WATAMBIA USAJILI BORA