Home Habari za michezo KUELELEKA MECHI YA KESHO….STARS WAPEWA MBINU ZA KUFUZU AFCON MBELE YA ALGERIA…

KUELELEKA MECHI YA KESHO….STARS WAPEWA MBINU ZA KUFUZU AFCON MBELE YA ALGERIA…

Zimbwe, Kapombe na wengine watemwa Stars

SAFU ya ulinzi imeshikilia hatima ya Taifa Stars katika mchezo wake muhimu wa mwisho wa kuwania kufuzu fainali za Mataifa ya Afrika (Afcon) 2023, ugenini dhidi ya Algeria, kesho Alhamisi, huku Juma Pondamali akisema Stars ina nafasi.

Katika mchezo huo ambao ni wa mwisho wa kundi F la mashindano hayo ambao utachezwa kuanzia saa 4:00 usiku kwenye Uwanja wa Mei 19, 1956 jijini Annaba, Taifa Stars inayoshika nafasi ya pili kwenye kundi F, inahitaji angalau sare tu ili iweze kufuzu fainali za Afcon zitakazofanyika Ivory Coast mwakani.

Kumbukumbu ya mechi tano zilizopita baina ya timu hizo mbili ambazo zilichezwa huko Algeria inaonyesha kuwa safu ya ulinzi imekuwa na takwimu za kuruhusu wastani wa mabao matatu katika kila mchezo ingawa safu yake ya ushambuliaji mara kadhaa imekuwa ikijitutumua na kupachika bao.

Algeria imekutana na Taifa Stars mara tano ikiwa nyumbani ambako wenyeji wameshinda mara tatu na Stars kuambulia sare mara mbili (2-1, 1-1, 1-1, 7-0 na 4-1).

Timu hizo kiujumla zimekutana mara 12 ambapo Algeria imepachika bao kwenye mechi hizo zote huku Tanzania ikifumania nyavu katika michezo minane.

Katika mechi zote 12 ambazo zimekutana, Algeria imepachika mabao 29 ikiwa ni wastani wa mabao 2.4 kwa mechi wakati Stars imefumania nyavu mara 11 ikiwa ni wastani wa bao 0.9 kwa mchezo.

Kipa wa zamani wa Taifa Stars, Juma Pondamali alisema matokeo ya nyuma yasiwatishe wachezaji wa timu hiyo dhidi ya Algeria. “Tukijilinda vyema tunapita. Ulinzi ni suala la timu nzima. Inawezekana mabeki wakacheza vizuri lakini kama hawatopata sapoti ya timu nzima wataishiwa kulaumiwa tu.”

SOMA NA HII  KUHUSU KUSAINI NA YANGA AU SIMBA..MOSES PHIRI KAVUNJA MZIZI WA FITNA..KAANIKA UKWELI WOTE HAPA...