Home Habari za michezo MANULA BADO WIKI TATU TU SIMBA….KUANZA NA AL AHLY….

MANULA BADO WIKI TATU TU SIMBA….KUANZA NA AL AHLY….

Habari za Simba leo

SIMBA haijapoteza mchezo wowote msimu huu hadi sasa na inawezekana mambo yakawa mazuri zaidi baada ya kipa wao namba moja Aishi Manula kurejea uwanjani na daktari kusema bado wiki tatu.

Manula alikuwa nje ya uwanja tangu mwisho mwa msimu uliopita baada ya kupata majeraha ya nyama za paja, lakini sasa daktari wa timu hiyo, Edwin Kagabo amesema anahitaji wiki tatu tu kuungana na wenzake uwanjani, hali ambayo inaonyesha anaweza kuiwahi mechi ya ufunguzi wa michuano mipya ya African Football League (AFL) dhidi ya mabingwa mara 10 wa Afrika, Al Ahly ya Misri, Kwa Mkapa, Oktoba 20.

Simba inatakiwa kuwa na kikosi imara kutokana na kuwa na majukumu mazito msimu huu ikishiriki michuano sita tofauti ukianza na Ngao ya Jamii, Ligi Kuu Bara, Ligi ya Mabingwa Afrika, Kombe la Mapinduzi, Kombe la ASFC na michuano mipya ya pesa ya AFL ambayo awali iliitwa Super League.

Kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika, Simba itaanza dhidi ya Power Dynamos ya Zambia Septemba 16 mwaka huu huko Kitwe Zambia, kisha Oktoba 20 itawaalika Al Ahly kwenye Uwanja wa Mkapa Dar es Salaam, kabla ya kucheza michuano ya Azam Federation na Kombe la Mapinduzi.

Manula pamoja na kuanza mazoezi mepesi ya uwanjani na wenzake lakini tangu Julai alikuwa ameanza mazoezi binafsi ya gym huku akionekana kurejea haraka kuliko matarajio.

“Sio kwamba makipa waliopo hawana uwezo wa kudaka, lakini Manula kwa mujibu wa wataalamu wetu ni kuwa anaendelea vizuri na anaweza kudaka mechi dhidi ya Al Ahly ingawa bado tutakuwa tukifanya mawasiliano na daktari kujua maendeleo yake ya kila siku.

“Tunataka kufanya vizuri kwenye mashindano haya, ndiyo maana tunaweka mikakati mizito ya kuhakikisha kila kitu kinakwenda vizuri, Manula alitakiwa arudi rasmi Novemba lakini hali yake sasa inaendelea vizuri tu,” alisema kiongozi huyo.

Kiongozi huyo alisema kuwa moja ya mambo yaliyojadiliwa kwenye vikao vyao vilivyofanyika kwa siku mbili juzi Jumapili na jana Jumatatu ni kuhusu michuano hiyo mikubwa miwili iliyo mbele yao.

“Kuna mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Power Dynamos tunaanzia ugenini, halafu Super Cup yote hatutaki kuishia njiani ndiyo maana tunajipanga kwa kila namna.”

Alipotafutwa Kagabo ili kujua maendeleo ya Manula na kama inawezekana kipa huyo kukaa golini mwezi ujao alisema;

“Maendeleo yake yanaridhisha kwa kiasi kikubwa. Sasa anaweza kufanya mazoezi ya kimpira na akiwa tayari tutawajuza lakini baada ya wiki mbili hadi tatu huenda akawa tayari kujiunga na wenzake.”

Kwa hesabu za haraka kwa mujibu wa maelezo ya Kagabo, basi Manula anaweza kuiwahi mechi hiyo ya Waarabu.

SOMA NA HII  SIMBA YAITAJA AZAM FC KUWA NJIA YAO KUFIKA FAINALI