Home Habari za michezo MASHABIKI WA POWER DYNAMO WATINGA DAR

MASHABIKI WA POWER DYNAMO WATINGA DAR

Mashabiki wa Klabu Bingwa nchini Zambia Power Dynamos wapo safarini kuelekea jijini Dar es salaam kwa ajili ya kuishangilia timu yao, itakayokabiliwa na mchezo wa Mkondo wa pili wa kuwania kufuzu Hatua ya Makundi Ligi ya Mabingwa Barani Afrika, dhidi ya Simba SC.

Miamba hiyo itakutana Jumapili (Oktoba Mosi) katika Uwanja wa Azam Complex, Chamazi jijini Dar es salaam, huku ikikumbuka matokeo ya sare ya 2-2 yaliyopatikana kwenye mchezo wa Mkondo wa Kwanza uliopigwa Uwanja wa Levy Mwanawasa mjini Ndola, Zambia Jumamosi (Septemba 16).

Klabu ya Power Dynamos imethibitisha kusafiri kwa Mashabiki hao kupitia kurasa zake za Mitandao ya Kijamii, kwa kuweka picha inayowaonesha wakiwa safarini kwa njia ya barabara.

Hatua hiyo ni kama majibu kwa Mashabiki wa Simba SC ambao walisafiri kuelekea Ndola, Zambia kwa lengo la kuishangilia timu yao ikicheza ugenini na kuambulia matokeo ya sare ya 2-2.

Wakati Mashabiki wakiendelea na safari, Kikosi cha Power Dynamos kinatarajiwa kuwasili jijini Dar es salaam leo Alhamis (Septemba 28) kwa ndege ya shirika la ndege la Tanzania ‘ATCL’.

SOMA NA HII  RASMI....SIMBA NA VIPERS WAMALIZANA SAKATA LA KUMSAJILI MANZOKI...KITUO KINACHOFUATA NI HIKI HAPA...