Home Habari za michezo KAMA UTANI KIPA MRUNDI AIBUKIA KAMBINI KWA YANGA

KAMA UTANI KIPA MRUNDI AIBUKIA KAMBINI KWA YANGA

Kikosi cha Yanga kimeendelea kujifua kwenye Uwanja wa Avic Town, Kigamboni, jijini Dar es Salaam kwa ajili ya mechi zijazo ikiwemo ya Ligi Kuu dhidi ya Azam FC itakayochezwa Oktoba 25 mwaka huu huku kipa Mrundi Ndizeye Aime (21), akionekana kikosini hapo.

Kipa huyo ambaye kwa sasa ni mchezaji huru, msimu uliopita alikuwa kipa namba moja wa Klabu ya Aigle Noir ya Ligi Kuu Burundi iliyomaliza msimu ikiwa nafasi ya tano kwenye msimamo.

Mmoja kati ya wasimamizi wa kipa huyo (jina tunalo), ameliambia Mwanaspoti kipa huyo yupo Yanga kwaajili ya kuendeleza kiwango chake kwa makubaliano maalumu lakini bado hajasajiliwa.

“Kwa sasa yupo huru ndio maana umemuona pale. Hajasajiliwa bali yupo kupata uzoefu na kutunza kipaji chake lakini kama atahitajika anaweza kusajiliwa,” alisema.

Uwepo wa Ndizeye kikosini hapo kunaifanya Yanga kuwa na makipa wawili wenye uzoefu, yeye na Aboutwalib Mshery huku wengine wakiwa vijana kutoka timu akademi ya kikosi hicho.

Djigui Diarra ambaye ni kipa namba moja wa Yanga, yupo kwenye kikosi cha timu yake ya taifa ya Mali sawa na Metacha Mnata aliye Timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ inayojiandaa na mechi ya kirafiki dhidi ya Sudani itakayopigwa Oktoba 15 mwaka huu kule Saudi Arabia.

SOMA NA HII  ROBERTINHO MLETENI YEYOTE TUPO TAYARI,.... ATAMBA BAADA YA KUKAA WIKI MBILI UTURUKI, MAYELE ASEPA RASMI YANGA