Home Habari za michezo LEO NDIO LEO DROO YA CAF HAPA SIMBA PALE YANGA…… UPI UTABIRI...

LEO NDIO LEO DROO YA CAF HAPA SIMBA PALE YANGA…… UPI UTABIRI WAKE

Habari za Michezo

Kabla ya kivumbi cha Coastal na Azam leo usiku pale Tanga, Simba na Yanga zitakuwa kwenye mijadala mizito. Droo ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika itachezwa leo saa 10 jioni nchini Afrika Kusini ambako kila mmoja atakuwa ameshajua Novemba 24-25 ataanzia mguu gani.

Droo hiyo itaanza na makundi ya Shirikisho saa 8 mchana ambapo kwenye eneo hilo hakuna timu ya Tanzania iliyofuzu. Timu 16 kati ya 54 kutoka vyama 42 vya soka Afrika vimepenya hatua hiyo ya makundi baada ya kushinda katika mechi za raundi ya pili, Yanga ikifuzu kwa mara nyingine baada ya kupita miaka 25 tangu ilipocheza mara ya kwanza mwaka 1998 michuano hiyo ilipobadilishwa kutoka Klabu Bingwa Afrika kuwa Ligi ya Mabingwa.

Yanga iliwang’oa Al Merrikh ya Sudan huku Simba ikifuzu kwa kanuni ya bao la ugenini dhidi Power Dynamos ya Zambia.

Matokeo hayo yamezifanya timu hizo kwa mara ya kwanza kutinga hatua hiyo katika michuano hiyo, zikiungana na miamba mingine 14 ya Etoile du Sahel na Esperance za Tunisia, Wydad Casablanca ya Morocco, Al Ahly na Pyramids za Misri na Al Hilal ya Sudan.

Pia kuna Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini, Petro Atletico ya Angola, Medeama ya Ghana, FC Nouadhibou ya Mauritania, TP Mazembe ya DR Congo, Jwaneng Galaxy ya Botswana, Asec Mimosas kutoka Ivory Coast na CR Belouizdad ya Algeria.

VYUNGU VINNE Cha kwanza kina Al Ahly, Wydad, Esperance na Mamelodi, huku Simba, Petro Atletico, CR Belouizdad na Pyramids zikiwekwa chungu cha pili, wakati kile cha tatu ni Yanga, TP Mazembe, Asec Mimosas na Al Hilal.

Chungu cha mwisho kina timu za Etoile Sahel, Jwaneng Galaxy, Medeama na Nouadhibou ikiwa ni kulingana na idadi ya pointi ilizokusanya kila moja na kanuni zinazuia timu za chungu kimoja kukutana, hii ikiwa na maana Simba na Yanga zilizopo vyungu tofauti zina nafasi ya kupangwa pamoja na wapinzani waliopo kwenye vyungu vingine au zisipate kukutana hadi hatua ya robo fainali iwapo zitafika huko.

ZITAKUTANA? Yanga na Simba kuwepo chungu tofauti zinaweza kupangwa katika makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa mara ya kwanza na kwa mujibu wa kanuni inaeleza wazi hakuna zuio la timu kutoka nchi moja kukutana.

Haitokuwa jambo la kushangaza ikiwa Yanga na Simba zitakutana katika hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwani imeshawahi kutokea mara nyingi tu huko nyuma kwa timu za nchi moja kukutana katika hatua hiyo.

Tangu hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika ianzishwe rasmi 1998, misimu 10 tofauti imeshuhudiwa timu za nchi moja kukutana katika hatua ya makundi. Kuna uwezekano wa timu tatu zilizokuwa kundi D la Kombe la Shirikisho Afrika mwaka 2016, Yanga, TP Mazembe na Medeama kukutana tena katika Ligi ya Mabingwa Afrika msimu huu.

Katika kundi hilo Yanga na Medeama zilishindwa kusonga mbele baada ya kumaliza katika nafasi mbili za mwisho, huku TP Mazembe ikiungana na MO Bejaia kutoka Libya kutinga hatua iliyofuata ambayo ilikuwa ni nusu fainali.

Hii itakuwa ni nafasi nyingine kwa Yanga kulipa kisasi kama itapangwa tena na Medeama ya Ghana kwani mwaka huo katika mchezo wa kwanza uliopigwa jijini Dar es Salaam Julai 16, 2016 ililazimishwa sare ya bao 1-1.

Katika mchezo wa marudiano uliopigwa Ghana wiki moja baadae ya Julai 26 mwaka huo, Yanga ilishindwa kutamba kwani ilichapwa mabao 3-1 na kuvuna pointi moja tu kati ya sita pindi ilipokutana na miamba hiyo.

Mbali na Medeama ila Yanga inaweza pia kupangwa na Al Hilal ya Sudan ambao nayo iliwatupa nje kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika msimu uliopita raundi ya kwanza tu baada ya kuifunga jumla ya mabao 2-1, Oktoba mwaka jana.

Licha ya kufanya vibaya katika Ligi ya Mabingwa ila msimu huo ndio ambao umekuwa wa kihistoria zaidi kwa Yanga kwani ilifika fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika na kupoteza kwa kanuni ya bao la ugenini dhidi ya USM Alger ya Algeria.

Yanga pia inaweza kupata fursa ya kulipa kisasi kwa Pyramids FC iliyowatupa nje katika hatua ya mchujo ya Kombe la Shirikisho Afrika baada ya kuifunga nyumbani na ugenini kwa jumla ya mabao 5-1, Oktoba 2019.

Kwa upande wa Simba inaweza kukutana na mechi nyingi za visasi ikiwa itapangwa katika kundi moja na baadhi yao huku Al Ahly ya Misri na Asec Mimosas ya Ivory Coast zikiwa miongoni mwao ambazo zilishawahi kukutana. Aidha inaweza kukutana na Wydad iliyowatoa kwenye robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu uliopita mbali na uwezekano mkubwa wa kukutana naMazembe iliyowatoa robo fainali msimu wa 2018-19.

Simba inaweza pia kupangwa na Jwaneng Galaxy iliyopo chungu cha nne iliyowatoa katika raundi ya kwanza tu ya Ligi ya Mabingwa msimu wa 2021/2022 kwa faida ya bao la ugenini baada ya kufungana mabao 3-3.

Akizungumza na Mwanaspoti juu ya droo hiyo, Kocha wa Simba, Roberto Oliveira ‘Robertinho’ alisema; “Kila mmoja wetu anatambua jinsi gani ambavyo tuna michezo mikubwa na migumu mbeleni ila kwangu kama kocha, wachezaji na viongozi tunajua njia bora ya kututimizia malengo yetu ni maandalizi,” alisema Robertinho aliyeifikisha Simba robo fainali msimu uliopita, huku kocha wa Yanga, Miguel Gamondi akikiri timu yake ipo tayari kukutana na mpinzani yoyote.

“Ukishafika hatua kama hii huna uchaguzi wa kupangwa na nani, lakini bahati nzuri timu ipo vizuri na ilishajua mapema imefuzu makundi na itakuwa tayari kupambana kusonga mbele zaidi, kwani mashabiki wana kiu ya kuona kile kilichotokea Kombe la Shirikisho msimu uliopita kinajirudia tena Ligi ya Mabingwa.”

Mechi za hatua ya makundi zitaanza kuchezwa rasmi kati ya Novemba 24 hadi 26. Mechi za makundi zitamalizika Machi mwakani. Kwa sasa Al Ahly ndio watetezi wa taji hilo ikitwaa msimu uliopita kwa kuwafunga waliokuwa mabingwa, Wydad kwa jumla ya mabao 3-2, hilo likiwa taji la 11.

MABINGWA Al Ahly SC (Misri) Al Hilal (Sudan), Asec Mimosas (Ivory Coast), CR Belouizdad (Algeria), ES Sahel (Tunisia), Esperance (Tunisia), FC Nouadhibou (Mauritania), Jwaneng Galaxy (Botswana), Mamelodi Sundowns (Afrika Kusini), Medeama SC (Ghana), Petro de Luanda (Angola), Pyramids (Misri), Simba SC (Tanzania), TP Mazembe (DR Congo), Wydad AC (Morocco), Young Africans (Tanzania).

SHIRIKISHO Abo Selim, (Libya), Al Hilal Benghazi (Libya), APC Lobito (Angola), Club Africain (Tunisia), Diables Noirs (Congo), Dreams FC (Ghana), Future FC (Misri), RS Berkane (Morocco), Sagrada Esperanca (Angola), Sekhukhune United (Afrika Kusini), Stade Malien (Mali), SuperSport United (Afrika Kusini), SOAR (Guinea), Rivers United (Nigeria) USM Alger (Algeria), Zamalek (Misri).

SOMA NA HII  ALICHOKISEMA KOCHA MPYA SIMBA, BAADA YA KUTAMBULISHWA