Home Habari za michezo BAADA YA KUMALIZANA NA JWANENG…..HUKO SIMBA BENCHIKHA NDIO KWAANZA KUNAKUCHA…

BAADA YA KUMALIZANA NA JWANENG…..HUKO SIMBA BENCHIKHA NDIO KWAANZA KUNAKUCHA…

Habari za Simba leo

Baada ya mapumziko mafupi ya kushangilia kutinga Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa kuichapa Jwaneng Galaxy mabao 6-0, mastaa wa Simba SC wamerejea mazoezini na kukutana na msala kutoka kwa kocha mkuu, Abdelhak Benchikha.

Kikosi kizima cha Simba SC kilichosheheni mastaa wakiwemo Clatous Chama na Saidi Ntibazonkiza ‘Saido’ walioonyesha kiwango bora kwenye mechi iliyopita dhidi ya Jwaneng walipofika kambini wamepewa msala na Benchikha wa kuhakikisha wanakusanya alama 12 katika mechi nne zijazo za ligi bila kuweka kisingizio cha aina yeyote.

Mastaa hao watakutana na ugumu kutokana na ratiba ya mechi hizo nne ilivyo kwani zitachezwa ndani ya siku saba pekee ambapo tatu zitakuwa nyumbani na moja ugenini.

Simba SC itaanza nyumbani kesho Jumatano (Machi 06) dhidi ya Tanzania Prisons mchezo utakaopigwa kwenye Uwanja wa Jamhuri Morogoro, sehemu ambayo Simba SC imechagua kucheza mechi zake za nyumbani kisha itasafiri kwenda Tanga ambako Jumamosi, Machi 9, itajitupa kwenye Uwanja wa Mkwakwani kupambana na Coastal Union kabla ya kurudi Morogoro kucheza mechi mbili dhidi ya Singida Fountain Gate, Machi 12 na Mashujaa, Machi 15, mwaka huu.

Bechikha amesema mechi hizo ni muhimu sana kwa Simba SC kwa kuwa zitaweka muelekeo wa ubingwa na lengo ni kukusanya alama zote 12, bila kujali wachezaji watakuvwa katika hali gani.

Kocha huyo anaamini kutakuwa na uchovu kwa baadhi ya wachezaji na wengine watakosa muda wa kutosha kupumzika lakini ni lazima wapambane ili kushinda zote.

“Nawapongeza sana wachezaji wangu kwa kile walichofanya katika mechi iliyopita (dhidi ya Jwaneng). Sasa tunarejea kwenye ligi, mpango ni kushinda mechi zote zilizo mbele yetu ili kuendelea kuwa katika nafasi nzuri ya kutwaa ubingwa.

“Ni wakati ambao wachezaji wanapaswa kujitoa zaidi, kutakuwa na uchovu lakini wanapaswa kupambana kwa ajili ya nembo ya Simba SC, tutajitahidi kufanya mabadiliko kadri tutakavyoweza ili kuleta uwiano lakini kubwa zaidi ni utayari wa kila mmoja kutimiza majukumu yake,” amesema Benchikha

Hadi sasa Simba SC ipo nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi na alama 36 ilizovuna kwenye mechi 15 ilizocheza nyuma ya vinara Young Africans wenye alama 43 baada ya mechi l6 sawa na Azam FC yenye alama 43 ilizopata kwenye mechi 19.

Kwa upande wa chipukizi, Ladack Chasambi (19) amesema amefurahia kufunga bao la kwanza katika Ligi ya Mabingwa Afrika, na sasa anapiga hesabu za kuendeleza moto huo kwenye mechi zijazo za Ligi Kuu.

SOMA NA HII  MASTAA HAWA SIMBA, WYDAD KUUKOSA MCHEZO WA MARUDIANO KWA MKAPA