Home Habari za michezo KUELEKEA DABI LEO….JULIO AFUNGUKA ALIVYOIKOA SIMBA NA AIBU…”NILIMFUKUZA MATOLA”….

KUELEKEA DABI LEO….JULIO AFUNGUKA ALIVYOIKOA SIMBA NA AIBU…”NILIMFUKUZA MATOLA”….

Habari za Michezo

Unaikumbuka ile #KariakooDerby ya Oktoba 2013 iliyomalizika kwa sare ya 3-3? Aliyekuwa Kocha Msaidizi wakati huo, Jamhuri Kihwelu ‘Julio’ amefunguka namna alivyochimba ‘biti’ wakati wa mapumziko na kipindi cha pili Simba ikasawazisha magoli matatu waliyofungwa na Yanga kipindi cha kwanza.

Julio amesema ilibidi awafanyie vurugu sambamba na maneno ya vitisho kwa wachezaji wake wakati wa mapumziko ambapo Mnyama alikua nyuma kwa bao 3-0.

Julio anasema alifukuza kila kiongozi aliyeingia kwenye vyumba vya kubadilisha nguo na aliwaambia wachezaji kuwa iwapo wangefungwa hakuna mchezaji ambaye angerejea tena kuichezea Simba huku akiwaambia angewakodia wahuni Wilayani Temeke wawadhuru ili wakajifunze.

Baada ya vitisho hivyo wachezaji wakarejea na moto mkubwa na kusawazisha mabao yote matatu na kuondoka na sare dhidi ya Yanga iliyokua bora zaidi kipindi hicho mwaka 2013.

“Bila kutarajia kipindi cha kwanza tukajikuta tumefungwa goli tatu za haraka na za kizembe! Sithibitishi, lakini zilikuwa zina hujuma ndani yake.”

“Tulipokwenda mapumziko, Kocha Abdallah Kibaden ‘King Mputa’ alikuwa analia! Mimi mwenyewe nilikuwa nalia lakini Mungu alinitia nguvu sikuongea ila nilifanya vurugu za kila aina.”

“Matola wakati huo alikuwa kocha wa timu ya vijana, alikuja dressing room akataka kuongea nikamtoa mbio! Akaja Basena ambaye ni rafiki mkubwa wa Geofrey Nyange ‘Kaburu’ na yeye nikamtoa mbio.”

“Baada ya kutukana nikawaambia wachezaji wa kigeni, mnatufanyia uhuni lakini labda baada ya mechi hii muondoke! Mimi ni Muhehe wa Iringa kama mtacheza tena mpira, mimi nitarudi tumboni kwa mama yangu hivihivi nilivyo.”

“Kama hii mechi tutapoteza mimi nitakodi wahuni wa Temeke, mtarudi kwenu mkiwa maiti kwenye maboksi. Baada ya maneno hayo wakatafakari wakaona huu moto, tukarudi uwanjani ukapigwa mpira tukasawazisha [Simba 3-3 Yanga].”

Vipi wadau Banchikha naye akopi na kupesti hii mbinu?

SOMA NA HII  MO DEWJI AWAPIGIA 'SALUTI' GOMES NA MATOLA