KUREJEA kwa nyota wawili wa Simba SC, Jonathan Sowah na Alassane Kante, kumempa ahueni Kocha Mkuu wa timu hiyo, Steve Barker, katika kusuka kikosi chake kuelekea mchezo wa Kariakoo Derby unaosubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki wa soka nchini.
Mchezo huo unatarajiwa kuchezwa Machi Mosi katika Uwanja wa New Amaan Complex, visiwani Zanzibar.
Sowah na Kante watakuwa sehemu ya kikosi hicho baada ya kumaliza adhabu yao ya kufungiwa, jambo linaloongeza chaguo na ushindani ndani ya timu kuelekea dabi hiyo ya watani wa jadi.
Awali, nyota hao walifungiwa michezo mitano na kesho Simba itakaposhuka dimbani kuvaana na Tanzania Prisons, watakuwa wanahitimisha adhabu yao rasmi. Hivyo, baada ya mchezo huo, watakuwa huru kurejea kikosini na kuanza kutumika katika michezo inayofuata.
Meneja wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally, amethibitisha kuwa wawili hao hawatakuwepo katika mechi dhidi ya Tanzania Prisons kwa kuwa wanakamilisha adhabu zao, lakini watarejea mara moja baada ya hapo.
“Baada ya mechi ya Tanzania Prisons, nyota hao watakuwa wamemaliza adhabu yao. Katika mchezo dhidi ya Dodoma Jiji FC watakuwa sehemu ya kikosi, na pia watakuwepo kwenye Kariakoo Derby pamoja na michezo mingine ijayo,” amesema Ahmed.
Katika hatua nyingine, Ahmed alizungumzia hali ya kipa namba mbili wa timu hiyo, Yakoub Suleiman, akieleza kuwa tayari yupo Dodoma na ameanza mazoezi mepesi.
Hata hivyo, uamuzi wa mwisho kuhusu kurejea kwake langoni utategemea majibu ya vipimo vya MRI vinavyosubiriwa kubaini kama yuko tayari kusimama golini au ataendelea kupewa muda zaidi wa kujiimarisha.