Home Habari za michezo ATLETICO, ARSENAL MECHI YA KUVIZIANA UEFA CL

ATLETICO, ARSENAL MECHI YA KUVIZIANA UEFA CL

0

MADRID, HISPANIA: Leo Atletico Madrid wataikaribisha Arsenal katika mchezo wa kwanza wa nusu fainali wa Ligi ya Mabingwa Ulaya utakaochezwa kwenye Uwanja wa Riyadh Air Metropolitano.

Huu ni mchezo mkubwa wa michuano hiyo baada ya jana kushuhudia mechi nyingine kali kati ya Bayern Munich na PSG.

Atletico wameshinda mechi 11 kati ya 15 za awali za mfumo wa nyumbani na ugenini dhidi ya timu za England katika mashindano ya Ulaya, ikiwemo nusu fainali zote tatu walizowahi kucheza. Hata hivyo, Arsenal waliwachapa 4-0 katika hatua ya ligi msimu huu na wanawapa mtihani mkubwa zaidi hadi sasa dhidi ya timu bora kutoka Ligi Kuu England.

Mchezo huu wa kwanza unaleta mvutano wa kipekee kati ya timu mbili zinazocheza soka kwa mtindo ambao haukuwa kawaida kwao kwa miaka ya nyuma. Atletico wamekuwa na nguvu kubwa ya ushambuliaji, wakifunga mabao 34 katika mashindano ya msimu huu, rekodi yao bora kabisa katika historia ya mashindano haya. Kwa upande mwingine, Arsenal wamekuwa imara sana katika safu ya ulinzi, wakiruhusu mabao matano tu katika michezo 12.

Safari zao za kufika nusu fainali pia zilikuwa tofauti kabisa. Atletico walikuwa na pambano kali dhidi ya Barcelona, wakishinda 2-0 katika mchezo wa kwanza, kisha kupoteza 2-1 katika marudiano kwa bao la Ademola Lookman. Arsenal wao waliifunga Sporting CP kwa jumla ya bao 1-0, baada ya ushindi mwembamba ugenini uliopatikana kwa bao la kuchelewa la Kai Havertz na kisha kulinda sare ya bila mabao nyumbani hali iliyowafanya kufika hapa walipo.

VIKOSI VINAVYOTARAJIWA:

Atletico: Oblak; Molina, Pubill, Le Normand, Ruggeri; Simeone, Llorente, Koke, Álex Baena; Griezmann, Alvarez

Arsenal: Raya; White, Gabriel, Saliba, Hincapié; Rice, Ødegaard, Zubimendi; Saka, Gyökeres, Martinelli

KAULI ZA MAKOCHA:

“Tunaingia nusu fainali kwa hamasa kubwa na imani kamili. Tunajua uwezo wetu na udhaifu wetu. Tuna imani kubwa na kile tunachofanya, tuko tayari na tunakwenda kupigania kile ambacho tumekuwa tukikifuatilia kwa miaka mingi,” amesema Diego Simeone kocha wa Atletico Madrid.

Mshambuliaji wa Atletico Antoine Griezmann amesema: “Haijalishi tunakutana na nani mradi bado tupo kwenye mashindano. Ilikuwa mechi ngumu dhidi ya Barcelona, lakini bado tupo.”

Kocha wa Arsenal Mikel Arteta amesema: “Ni hatua kubwa sana kufika nusu fainali mfululizo. Ni mara ya kwanza katika historia yetu ya miaka 140. Lazima ufanye kazi kubwa kufika hapa.”

Mshambuliaji wa Arsenal Gabriel Martinelli amesema: “Tunaamini katika uwezo wetu. Tulishawafunga katika hatua ya ligi, lakini hii itakuwa mechi tofauti kabisa.”

MATARAJIO

Timu mbili zenye matumaini makubwa zinakutana katika mchezo huu wa kwanza wa nusu fainali. Kwa kuzingatia mitazamo ya makocha wote wawili, mechi hii inatarajiwa kuwa ya kimkakati zaidi, huku kila upande ukijaribu kupata faida kabla ya dakika 90 za marudiano jijini London.

Ingawa Arsenal waliwahi kushinda katika hatua ya ligi, Atletico wameimarika zaidi tangu wakati huo, hasa katika safu ya ushambuliaji unaoweza kubadilisha mchezo wakati wowote kupitia wachezaji kama Julián Álvarez, Antoine Griezmann, Alexander Sørloth au Ademola Lookman. Si bahati mbaya kwamba kikosi cha Diego Simeone kina mojawapo ya safu bora za ushambuliaji katika mashindano haya lakini kinakutana na safu bora ya ulinzi.

DONDOO

Hii ni mara ya nne tu wanakutana kwenye mashindano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya kati ya Atlético Madrid na Arsenal. Hapo awali walikutana kwenye nusu fainali ya michuano hiyo msimu wa 2017/18 ambapo Atletico walishinda kwa jumla ya mabao 2-1 (1-1 London, 1-0 Madrid), na pia Arsenal walishinda 4-0 nyumbani katika Mechi ya 3 ya UEFA msimu huu.

Atletico wameshinda mechi mbili tu kati ya 12 zao za mwisho za UEFA dhidi ya timu za England (sare 2, kupoteza 8), lakini wamepoteza mechi mbili tu kati ya 18 walizocheza dhidi ya timu hizo wakiwa Madrid (ushindi 9, sare 7).

Atletico wameshinda mechi11 kati ya 15 za awali nyumbani na ugenini dhidi ya timu za England katika mashindano ya UEFA, ikiwemo nusu fainali zote tatu walizocheza: dhidi ya Liverpool katika Europa League 2009/10, Chelsea kwenye UEFA 2013/14, na Arsenal katika Europa 2017/18.

Timu hiyo ya Hispania imefuzu nusu fainali saba za UEFA, ikiwa imeshinda mara tatu na kupoteza mara tatu katika sita zilizopita. Mara ya mwisho ilikuwa 2016/17 walipopoteza kwa jumla ya mabao 4-2 dhidi ya Real Madrid, na mafanikio yao ya mwisho hatua hii yalikuwa 2015/16 walipowatoa Bayern Munich kwa sheria ya mabao ya ugenini.

Arsenal wameshinda mechi zao saba za mwisho za UEFA dhidi ya timu za Hispania, ikiwemo ushindi wa 4-0 dhidi ya Atletico kwenye mechi ya 3. Hii inawafanya kuwa timu ya kwanza katika historia ya mashindano hayo kushinda mechi saba mfululizo dhidi ya timu za Hispania. Pia wameshinda mechi zao nne za mwisho za ugenini dhidi ya timu za Hispania.

‘The Gunners” wameshinda mikondo mitano na kupoteza minne kati ya tisa za awali za hatua za nyumbani na ugenini dhidi ya timu za Hispania katika UEFA, Hii ni nusu fainali yao ya pili dhidi ya timu ya Hispania, ambapo walishinda dhidi ya Villarreal kwa jumla ya 1-0, msimu wa 2005/06.

Arsenal wamefika nusu fainali ya UEFA kwa msimu wa pili mfululizo, jambo la kwanza katika historia yao na hii ni nusu fainali yao ya nne kwa ujumla. Walishinda dhidi ya Villarreal mwaka 2005/06 kabla ya kupoteza mbili zilizofuata katika hatua hii dhidi ya Manchester United mwaka 2008/09 na Paris Saint-Germain msimu uliopita.

Timu hiyo ya London ndiyo pekee ambayo haijapoteza mechi yoyote katika Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu huu (ushindi 10, sare 2). Kwa ujumla, wamepoteza mechi mbili tu kati ya 22 za mwisho kwenye mashindano haya (ushindi 17, sare 3).

Arsenal wamepoteza mechi moja tu kati ya 11 za mwisho za ugenini katika Ligi ya Mabingwa Ulaya (ushindi 9, sare 1).